Labels

Tuesday, October 2, 2012

MPANGO WA MUNGU WA WOKOVU


Kuokoka ni jambo ambalo halieleweki vizuri kwa baadhi ya watu katika imani ya kikristo. Kuna wakristo wanaokataa na pengine  kudhihaki kuwa hakuna wokovu duniani na kwamba wanaoamini katika wokovu wamechanganyikiwa. Aidha utata mwingine katika suala la kuokoka ni pale ambapo baadhi ya watu wanaoamini kuwa wokovu upo wanapodai kwamba mtu hawezi kuokoka akiwa hai bali kuokoka ni baada ya kufariki dunia.

Hayo ni mawazo potofu na inasikitisha zaidi inapoonekana kuwa hata baadhi ya viongozi wa makanisa hawalielewi vizuri suala hili ambalo ni muhimu katika imani ya kikristo kwani ndiyo sababu hasa iliyomleta Bwana Yesu Kristo duniani, kuja kuwaokoa watu katika dhambi zao kama yasemavyo maandiko matakatifu kwamba; “Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi.” 1 Timotheo 1:15.  Kutoeleweka vizuri kwa suala hili matokeo yake ni watu kuyumba au kuyumbishwa kiimani, na hata baadhi ya wanaodhani wanaelewa maana yake wakijikuta wakiwa nje ya ukweli na hivyo maana nzima ya wokovu kupotoshwa.

 Kwa yeyote anayejiita mkristo lakini anakataa kwamba hakuna wokovu ajue kwamba hana haki ya kujiita mkristo. Kwani Ukristo siyo kuwa na majina yanayoitwa ya ‘kikristo’ au labda  kula baadhi ya vyakula ambavyo imani nyingine inakataza kula; bali Ukristo ni imani ambayo ni Yesu mwenyewe kama yasemavyo maandiko kuwa; Lakini kabla ya kuja ile imani tulikuwa tumewekwa chini ya sheria, tumefungwa mpaka ije ile imani itakayofunuliwa. Hivyo torati imekuwa kiongozi kutuleta kwa Kristo, ili tuhesabiwe haki kwa imani. Lakini iwapo imani imekuja, hatupo tena chini ya kiongozi.”  Wagalatia 3:23-25.

Wokovu unapatikana kwa Yesu Kristo pekee kwa kuwa Yeye ndiye njia pekee ya wokovu. Mlinzi wa gereza walimokuwa wamefungwa Paulo na Sila baada ya kushuhudia nguvu za Mungu aliwauliza Paulo na Sila afanyeje ili aweze kuokoka; “Kisha akawaleta nje akasema ‘Bwana zangu, yanipasa nifanye nini nipate kuokoka?’ wakamwambia ‘mwamini Bwana Yesu nawe utaokoka pamoja na nyumba yako” Mdo. 16:30-31.

Wokovu upo na ni kwaajili ya wanadamu walio hai na si vinginevyo. Biblia takatifu inafundisha kuhusu wokovu. Yaani maana nzima (main theme) ya Neno la Mungu ni Wokovu. Injili inahubiriwa duniani kote ili watu wamjue Mungu kisha waokoke, na wokovu unapatikana kabla ya mtu hajafariki dunia. Bwana Yesu mwenyewe amelielezea suala hilo katika mfano alioutoa kuhusu maisha ya tajiri na maskini Lazaro ambapo baada ya wote kufariki, Lazaro alikwenda peponi na yule tajiri alikwenda motoni kulingana na matendo yao. Kwakuwa walikuwa wakionana wakiwa huko, yule tajiri kutokana na mateso  aliyokuwa akipata aliomba Lazaro atumwe duniani kuwaeleza ndugu zake tajiri jinsi hali ya mateso makali anayopata mtu asiyeokoka baada ya kufa kwake ilivyo, hivyo kuwataka ndugu zake hao watubu dhambi zao wakiwa huko huko duniani kwani hakuna nafasi ya kutubu baada ya kifo. (Luka 16:19-31).

 Wokovu unapatikana wakati mtu akiwa hai tu kwani baada ya kufa kinachofuata ni hukumu, hakuna uwezekano wa kuutafuta wokovu ukishakufa kwani maandiko yanasema; “Na kama vile watu walivyowekewa kufa mara moja, na baada ya kufa hukumu.” Waebrania 9:27. Dini zipo duniani ikiwa ni jitihada za wanadamu katika kumtafuta Mungu ili waokoke na kujiepusha na adhabu ya Mungu, kusingekuwa na sababu ya watu kupoteza muda wao makanisani na sehemu zingine za ibada kama kusingekuwa na matarajio ya kupata ujira wa wokovu, ingawa hata hivyo wokovu siyo dini bali ni imani.

Wokovu ni mpango mahususi wa Mwenyezi Mungu kwa wanadamu. Mungu alipomuumba mwanadamu alikusudia kumfanya asife, aendelee kuishi milele na kuwa karibu naye. Hata hivyo Adamu alipofanya dhambi ya kumwasi Mungu ndipo Mungu alipokasirika na kumfukuza Adamu katika bustani ya Edeni. Dhambi humtenganisha mwanadamu na Mungu hivyo alimwambia Adamu kwamba atakufa; “Kwa maana u mavumbi wewe nawe mavumbini utarudi.” Mwanzo 3:19.

Mwanadamu anakufa asipokuwa na Roho wa Mungu lakini akiwa na Roho wa Mungu kinachokufa ni mwili tu lakini Roho yake haifi. Adamu alipomwasi Mungu ndipo alipojikuta kwa mara ya kwanza akiwa uchi na akaanza kuwa na hofu; yaani hakuwa tena na ile Roho wa Mungu iliyomfanya ajiamini. Wanadamu vizazi kwa vizazi wakaendelea kumwasi na kumkasirisha Mungu. Kutokana na kukithiri kwa maasi, Mungu akaleta gharika kuu na kuwateketeza wote isipokuwa Nuhu na familia yake tu, kiburi cha mwanadamu hakikukoma; wakiwa chini ya kiongozi wao Nimrodi wanadamu wakaazimia kujenga mnara mrefu kwa matofali ya kuchoma huko Babeli ili wamfikie Mungu. Hata hivyo Mungu akawasambaratisha. Vilevile akaiteketeza miji ya Sodoma na Gomora kwa moto kutokana na kukithiri kwa maasi lakini akamsalimisha Lutu na wanawe tu. Hicho ndicho kiburi cha mwanadamu dhidi ya Mungu.

Ndipo Mungu alipochukizwa na kizazi cha wana wa Israeli akawapa adhabu kwamba kizazi chao kitakwenda utumwani Misri kwa muda wa miaka mia nne. Baada ya mateso mengi ya utumwani, wana wa Israeli walimlilia Mungu naye akasikia kilio chao ndipo alipokumbuka agano lake na Ibrahimu, na Isaka  na Yakobo kwamba kizazi chao kitakwenda utumwani Misri kwa muda wa miaka mia nne na baada ya hapo watarudi katika nchi yao ya ahadi, akaamua kuwaokoa kutoka  utumwani kupitia kwa Musa na kuwarejesha katika nchi aliyowaahidi mababu zao.

No comments: