Labels

Wednesday, October 10, 2012

KWA NAMNA GANI MTU ANAWEZA KUMZIMISHA ROHO MTAKATIFU?


Roho Mtakatifuni Mungu, mwenye nguvu zote, maarifa yote, anayepatikana kila mahali. Yeye pia anayo nafsi na kwa hiari yake ameamua kuishi ndani ya mwili wa mwanadamu kwa kuzingatia mgawanyo wa majukumu waliyokubaliana yaani nafsi ya    Mungu Baba, Mungu Mwana(Yesu) na Mungu Roho Mtakatifu. Kazi/lengo kubwa la ujio wake ni kuwa Msaidizi wa mwanadamu kwenye ulimwengu huu wa mwili, ili kumsaidia kuishi katika mapenzi ya Mungu.
Mungu hana namna ya  kutawala kwenye ulimwengu wa kimwili bila kuwa na mwili wa damu na nyama, kwa kuwa yeye ni Roho (Yohana 4:24). Hivyo hana budi kuingia kwenye mwili wa mtu na kufanya makao yake hapo, ili kutawala na kumuongoza mwanadamu katika mapenzi yake (Yohana14:18, 23, 1Wakorinto 3:16-17, 6:19). Kwa sababu hii ni muhimu sana kwetu kutunza mahusiano yetu na Roho Mtakatifu ili tusimzimishe katika maisha yetu.
Paulo akizungumza na ndugu wa Thesalonike alisema ‘Msimzimishe Roho’ (1Wthesalonike 5:19). Paulo alitoa maonyo haya kwa kuwa alijua, Kumzimisha Roho Mtakatifu, kuna athari mbaya sana kwenye maisha ya mwamini katika kulitumikia kusudi la Mungu na hata maisha yake ya kawaida hapa duniani. Swali la msingi ni, kwa namna gani mtu anaweza kumzimisha Roho Mtakatifu? Ukisoma tafsiri za kiingereza, Biblia ya toleo la GNB katika mstari huu inasema Do not restrain the Holy Spirit’ na toleo la KJV linasema ‘Quench not the Spirit’ (1Th 5:19).
Tafsiri hizi mbili zinapanua zaidi tafsiri ya kumzimisha Roho, katika dhana mbili zifuatazo; moja kumzimisha Roho ina maana ya kumzuia Roho Mtakatifu asitawale na kuongoza maisha yako kwa kukataa msaada wake maishani mwako. Pili, kumzimisha Roho Mtakatifu ina maana ya kuishi katika mazingira ambayo yanamfanya Roho Mtakatifu ashindwe kukusaidia.
Mazingira ambayo Roho Mtakatifu anaweza kuzimishwa;
  • Kutokumpa nafasi akusaidie
Kwa mujibu wa Matahayo 14:16, Roho Mtakatifu ameletwa kwetu kama Msaidizi. Kwa tafsiri, Msaidizi ni yule atoaye msaada pale anapohitajika na kupewa nafasi ya kufanya hivyo. Vivyo hivyo na Roho Mtakatifu kama hujampa nafasi ya kukusaidia (ingawa yupo ndani yako), hawezi kufanya hivyo na kwa hiyo taratibu utakuwa unamfungia/unamzuia kukusaidia maishani mwako.
  • Kukosa upendo
Ukisoma kitabu cha 1Wakorinto sura ya 13 na 14, utagundua kwamba suala la upendo limepewa msisitizo wa kipekee kwa mtu ambaye anataka kuona utendaji wa kazi wa Roho Mtakatifu kwenye maisha yake na kwa ajili ya wengine pia. Upendo kwa mtu aliyejazwa Roho Mtakatifu ni moja ya vigezo muhimu sana kwa Roho Mtakatifu kusema/kujifunua na kufanya kazi ndani yako. Hivyo kukosa upendo ni dalili ya kumzimisha Roho Mtakatifu ndani yako. Ndiyo maana Paulo anasema hata kama angekuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, pia kuwa na imani timilifu kiasi cha kuhamisha milima, kama hana upendo si kitu yeye, naam ni bure tena ni ubatili (1Wakorinto 13:1-3).
  • Kuongozwa au kuenenda kwa mwili
Paulo aliwaambia hivi wandugu wa Galatia ‘Basi nasema, Enendeni kwa kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili’ (Wagalatia 5:16). Maneno haya alikuwa akiwaambia watu waliokoka na si wasiomjua Mungu. Kanisa la Galatia lilikuwa limeacha kuenenda kwa Roho likaanza kuenenda kwa mwili. Paulo akajua jambo hili litamzimisha Roho wa Bwana ndani yao, na kwa sababu hii hawataweza kuishi maisha ya ushindi hapa duniani na kisha kuurithi uzima wa milele, ndipo akawaonya akisema enendeni kwa Roho ili msizitimize tama za mwili.
  • Kutokutii maelekezo yake
Roho Mtakatifu kuitwa Msaidizi haina maana tunapaswa kumpamngia cha kufanya. Yeye ndiye mwenye kutuongoza katika njia itupasayo kuiendea (Zaburi 32:8). Kinachotakiwa ni mtu kuwa mtiifu kwa yale ambayo Roho Mtakatifu anakuagiza. Kukosa utiifu mara kwa mara kila anapokusemesha/kukuagiza ni kumjengea mazingira ya kutoendelea kusema na wewe na hivyo kuondoka kwako na kutafuta mtu mwingine amtumie kwa kusudi lake. 
  • Kukosa ufahamu wa utendaji wake
Mara nyingi watu wamemzimisha Roho kwa kutokujua utendaji wake ulivyo. Kuna nyakati Roho Mtakatifu anaweza akaleta msukumo ndani ya mtu wa kumtaka aombe, atulie kusoma neno n.k. Lakini kwa kutokujua namna anavyosema, wengi hujikuta badala ya kutulia na kufanya kile alichopaswa kufanya, wao hufanya mambo mengine.
Pia kuna nyakati katika ibada (sifa, maombi nk), Roho Mtakatifu anaweza akashuka juu ya mtu au watu na akataka kusema jambo, lakini viongozi wa makanisa au vikundi husika wakawazuia hao watu. Kufanya hivyo bila uongozi wa Mungu ni kumzimisha Roho. Mandiko yako wazi kabisa kwamba hatupaswi kutweza unabii (1 Wathesalonike 5:20) na wala hatupaswi kuzuia watu kunena kwa lugha (1Wakorinto 14:39). Zaidi tumeagizwa kujaribu mambo yote, na tulishike lililo jema (1 Wathesalonike 4:21).
Je tutajaribuje mambo yote ikiwa tunawazuia watu Kunena na pia tunatweza unabii? Hofu yangu ni kwamba kwa kuzuia watu kunena na pia kutweza unabii tunaweza tukajikuta tunamzimisha Roho Mtakatifu na kukataa uongozi wake kwenye maisha yetu. Ni vema tukakumbuka kile ambacho Paulo aliwaambia Wakorinto juu ya mambo haya kwamba ‘mambo yote yatendeke kwa uzuri na kwa utaratibu’ (1 Wakorinto 14:40). Naam na hili lina maana ni vema kwanza ujue utendaji wa Roho Mtakatifu ukoje, ili kuepuka kumzimisha kwa kutokujua utendaji wake.
Pengine yapo mazingira mengine ambayo mtu anaweza akajikuta anamzimisha Roho Mtakatifu. Kumbuka jambo hili kwamba kumzimisha Roho Mtakatifu ni kumzuia asikusaidie, jambo ambalo tafsiri yake ni kukataa uongozi wake kwenye maisha yako. Biblia inasema katika Warumi 8:9 ‘Lakini ikiwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu, ninyi hamwufuati mwili; bali mwaifuata roho. Lakini mtu awaye yote asipokuwa na Roho wa Kristo huyo si wake’. Usifanye mchezo na Roho Mungu hakikisha unatunza sana mahusiano mazuri kati yako na yeye kwa kutokumzimisha.
Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo iwe nawe

No comments: