Labels

Monday, October 8, 2012

KUSIFU NA KUABUDU

                                                      na
                                         Meshack  Ezekia Kitova

Pamoja na ukweli huu wa sifa na kuabudu kuwa sehemu ya maisha ya mtu ya kila siku, bado kuna nguvu za ajabu pale waamini wanapomwimbia Mungu sifa. Huduma ya kumwimbia Mungu nyimbo za sifa na kuabudu, ndiyo huduma pekee ambayo mwamini hutumia nguvu na bidii nyingi, kupitia nafsi zake tatu. Kwanza, kupitia uimbaji mwamini hutumia nguvu kumpazia Mungu sauti yake, pili, hutumia viungo vya mwili wake kama vile mikono, miguu katika kucheza mbele za Mungu wa utukufu. Hali kadhalika katika kumwimbia Mungu sifa na kumwabudu, mwamini hutumia pia ufahamu kujihudhurisha mbele za Mungu mwenye maarifa yote. Bidii hizi zinazohusisha nafsi zote za mwanadamu, ndizo hatimaye zinazomleta mwamini karibu zaidi na nguvu na uwepo wa Mungu.
Katika kumsifu na kumwabudu Mungu, kanisa la Maranatha Reconciliation linaelewa kuwa, Roho Mtakatifu aliyemwagwa bila kipimo wakati wa Pentekoste ya kwanza baada ya ufufuko wa Bwana ni Roho wa sifa. Kiu yake kila wakati ni kuwaongoza waamini kumtolea Mungu sadaka ya sifa; mahali popote wanapokuwa ikiwa ni nyumbani, njiani, makazini, vitandani, kwenye maombi, wakati wa ibada n.k. Hata hivyo, kutokana na ukosefu wa mafundisho ya kutosha waamini wengi wameridhika na sifa na kuabudu kunakofanyika katika mikusanyiko ya ibada peke yake. Wakati umefika kwa watoto wa Mungu kuondoa vifusi vilivyoiangukia huduma hii na kuifanya ipoteze maana yake ya awali. Vifusi hivi vikishaondoka, kila mwamini katika nyumba ya Mungu atatambua kuwa, kusifu na kuabudu ni maisha na sio kuimba peke yake.
Hali kadhalika vifusi hivi vikishaondoka, waamini watatambua pia uhusiano uliopo kati ya kusifu na kumtolea Mungu shukrani. Ukiangalia mashairi ya mfalme Daudi, utagundua kuwa, nyingi ya Zaburi zake zinaongelea umuhimu wa kumtolea Mungu dhabihu za shukrani. Kwa mfano, tunapoangalia zaburi ya 116, tunakutana na shairi lifuatalo, "Nitakutolea dhabihu ya kushukuru; Na kulitangaza jina la BWANA." Zab 116:17. Katika kumsogelea Mungu ni sharti dhabihu hii ya shukrani itangulie kabla ya ile ya sifa na kuabudu. Ni katika hali ya kumtolea Mungu dhabihu ya shukrani ndipo Roho wa Mungu anapozimiliki nafsi tatu za mwamini na kumwongoza kumwadhimisha Bwana kwa bubujiko la ajabu, huku akitokwa na machozi ya furaha. Kutokana na uhusiano uliopo kati ya sifa, kuabudu na shukrani, ni sahihi kusema kuwa, ibada ya kweli ni lazima iwe na mambo makubwa matatu, KUABUDU, KUSIFU na KUSHUKURU.
Kwa maneno haya machache, tunayo imani kwa Mungu kuwa ataleta uamsho wa sifa na kuabudu kwa kweli katika kanisa lake hapa Tanzania. Wakati huu ambao uovu unaonekana kuimeza dunia, huduma hii ya kusifu na kuabudu kwa kweli, inahitajika sana katika kanisa. Huduma hii ndiyo itakayoweza kuziangusha ngome hizi za uovu. Ngome hizi zikishaanguka, ukuaji wa kanisa kitabia, kiidadi na kijiografia nao utashika kasi tofauti na ilivyo sasa. Mungu akubariki na akupe kiu na bidii ya kufanya huduma ya kusifu na kuabudu kuwa sehemu ya maisha yako ya kila siku. KILA MWENYE PUMZI NA AMSIFU BWANA, HALELUYA!

No comments: