Labels

Wednesday, October 10, 2012

MAKOSA WANAYOFANYA VIJANA KATIKA KUTAFUTA MWENZI WA MAISHA.

KWA NINI VIJANA WENGI WANAKOSEA KATIKA KUTAFUTA MWENZI WA MAISHA?
Maamuzi ya kuoa au kuolewa, si maamuzi madogo, ni moja ya maamuzi makubwa ambayo vijana wengi wa kike na wa kiume wana kutana nayo kila siku. Sasa katika kufanya maamuzi haya ukweli ni kwamba sehemu kubwa ya vijana mpaka wafike mahali pa kumpata kijana au binti wa kusema huyu ndiye haswa wa kutoka kwa Bwana, basi ujue tayari wengi wanakuwa walishakosea mara nyingi mpaka kufikia hapo. Wapo ambao wakikosea husema, yule wa kwanza hakuwa chaguo la Bwana, au haukua ufunuo wa Mungu mwenyewe bali malaika, au utasikia mwingine akisema Bwana amemchukia Esau akampenda Yakobo au amehamishia upako wa Sauli kwa Daudi kwa maana ya kwamba upako umehama kutoka binti wa kwanza hadi kwa mwingine. Mimi sina uhakika sana na hizi kauli.
Je hivi kweli hayo ndiyo yalivyo au ni ujanja ujanja tu wa vijana tena hasa wa kiume ndio wenye kauli kama hizi. Lengo la waraka huu mfupi kwako kijana mwenzangu ni kutaka kukueleza sababu kadhaa ambazo kupelekea vijana wengi kufanya makosa katika kutafuta mwenzi wa maisha.
*Wengi wanakuwa tayari wameshafanya maamuzi ya nani ataishi naye.Vijana wengi huwa wanaomba Mungu awape mtu sahihi wa kuishi naye na wakati huohuo tayari kwenye nafsi yake anakuwa na mtu wake kwamba lazima huyu tu ndiye nitaishi naye. Na kwa sababu hiyo ina kuwa ni vigumu kwao kumpata mtu wa mapenzi ya Mungu na pia ina muwia kazi Mungu kukuonyesha mke au mme wa kusudi lake kwani tayari umeshafanya maamzi ndani yako, je Mungu afanye nini kama sio kunyamaza.
*Sababu za kipepo
Hapa nitaelezea mambo mawili kwa wakati mmoja, la kwanza ni hili kuna vijana huenda wao wenyewe au ndugu zake, wazazi wake walishawahi kumtoa huyo mototo kama dhabihu kwa mapepo kwa sababu ya mila zao au pia alipatikana kwa njia za kipepo. Siri moja ni hii kuna baadhi ya mapepo huwa hayapendi kushare sex na mtu mwingine, hivyo ni lazima yalete kila namna ya upinzani ili mtu asiolewe na wala kuoa. Na mwingine hata kama hakutolewa kama dhabihu lakini huenda pepo wameshawahi kufanya mapenzi na huyo mtu na kama yatampenda basi ujue hayatakubali aolewe au kuoa, hivyo yatamletea kila namna ya upinzani katika kuolewa au kuoa kwake. Mengine hufika mahali hata pa kumwachia kijana wa watu harufu mbaya ili mwingine asimpende.
*Maneno ya kujitamkia
Kuna baadhi na hasa hapa ni akina dada kwa sababu mbalimbali kama vile kubakwa, kujeruhiwa katika nafsi kwa sababu ya kuachwa na mchumba wake hufikia mahali wakasema mimi sitaki tena kuolewa. Sasa inpofika muda umepita na wanataka tena kuolewa wananaza kuomba Mungu awape mume, wakati huo wamesahau kwamba walishatamka kwamba hawataki tena kuolewa. Nisikilize ukisema hutaki kuolewa au kuoa tena, maana yake unaifunga nafsi yako hapo kwamba hutaoa kuolewa, na Biblia inasema mtu atashiba matunda ya kinywa chake. Na wakati huo shetani ni mwepesi kufuatilia maneno ambayo ni ya athari kwako. Sasa bila kufuta kwa Damu ya Yesu ndugu utakesha hapo.
*Dhambi.
Sikiliza Biblia inasema afichaye dhambi zake hatafanikiwa, (Mithali 28:13a). Kuna baadhi ya vijana huwa wanakuwa awali kuna baadhi ya dhambi wamezifanya na hawajazitubia, na bado wana taka mtu awaoe au wa kumwoa. Biblia iko very clear kama kuna dhambi umeficha hutafanikiwa, sasa inategemeana, lakini pia inahusiana sana na kutofanikiwa kwako pia kumpata hata mwenzi tu. Nikupe mfano mara nyingi watu wanatoa mimba, au watoto wanaozaa, nao pia kupata mume au mke huwa inakuwa kazi kweli kweli.
*Kutokuenenda kwa Roho.Paulo anasema, “Basi nasema enendeni kwa roho wala hamtatimiza kamwe tama za mwili” (Wagalatia 5: 16). Kuenenda wa Roho maana yake ni kuongozwa na Roho Mtakatifu, hii ni pamoja na zoezi zima la kutafuta mke au mme. Sasa kwa sababu wewe unaenda kwa mwili, mara eti nataka mtoto portable, mguu wa chupa, mweupeee, nk. Hivyo vitu unavyotaka wewe kuna wengine pia wanataka hivyohivyo na matokeo yake mnaanza kugombaniana msichana au mvulana kwa sababu tamaa za miili yetu zinawaongoza huko.
*Kuwa na vigezo binafsi.
 Vijana wengi sana katika suala zima la kupata mke ua mme, ukweli wengi wao wana vigezo vingi sana ambavyo kila mmoja angependa huyo mchumba wake awe navyo. Utasikia lazima awe wa kabila ya kwangu, awe portable, mweupee, mrefu ndio mzuri, ajue kutabasamu na kisha awe ana ulamba. Sawa mi sikatai hivyo vigezo, lakini nikuulize swali Je! Unayajua mawazo ya Mungu kuhusu wewe kwa habari ya mkeo au mmeo? Je kibiblia hivyo vigezo vyako vinakubalika/ na je mke/mme mtu huchagua mwenyewe au hupewa na Bwana?
 Najua utaniambia mimi nitaomba Mungu anipe mke/mme mwenye sifa hizo. Ok. Ukiniambia hivyo na mimi nitakuambia kumuomba Mungu kwa muundo huo ni nzuri kabisa, wala sio dhambi lakini kumbuka maandalio ya moyo ni ya mwanadamu lakini jawabu la ulimi hutoka kwa Bwana. Na hapo ndipo patamu, wengi huwa wanaomba kwa vigezo vyao, na mara nyingi Mungu anapojibu inakuwa tofauti na vigezo vyao, na hapo wengine wanakataa hata chaguo la Bwana wanabakia kuteseka. Jua kwamba wewe unapoweka vigezo vya mwenzi wako na Mungu naye ana vigezo vya aina ya mwenzi anayekufaa.
* Kufanya maamuzi kabla ya wakati.
Biblia inasema katika Mhubiri 3:1 “kwa kila jambo kuna majira yake, na wakati wa kila kusudi chini ya mbingu”.Hili ni jambo la kawaida, hata wakati wa uchaguzi kura mtu harusiwi kupiga kama hajafikisha miaka kumi na nane kwa nchi nyingi. Vivyo hivyo hata suala la kutafuta mke au mume lina wakati wake maalumu. Ukitaka kulifanya nje ya kipindi ambacho Mungu amekipanga kwa ajili yako utateseka hadi uchoke. Kumbuka kila mtu ana muda wake, hivyo basi hakuna muda maalumu wa kila mtu kuanza kutafuta mke au mme, bali kila mtu ana muda wake na mara tu unapowadia Mungu humjulisha mtu wake.
Nisikilize ukiulekeza moyo wako upate kujua haya nisemayo na ukajizuia kufanya makosa kama haya, basi nataka nikuhakikishe suala la kupata mke au mme wa kutoka kwa Bwana litakuwa ni jepesi sana,ni sawa sawa na kuombea chakula na ukishafumbua macho ukaanza kula moja kwa moja ukiwa na uhakika kimeponywa na kubarikiwa.
Ndimi katika huduma hii,
Meshack.E.Kitova

MAMBO YA KUFANYA/KUZINGATIA KATIKA KIPINDI CHA UCHUMBA

Katika kitabu cha Muhubiri 3:1 Biblia inasema “Kwa kila jambo kuna majira yake, na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu”. Hivyo mwanadamu katika maisha yake hapa chini ya jua  kuna vipindi mbalimbali anavyovipitia hii ni pamoja na kipindi cha uchumba kwa sehemu kubwa ya watu.  
Katika kipindi hiki yapo mambo mengi ambayo wachumba hufanya, mengine ni mazuri na mengine hayafai kabisa. Na hii yote inatokana hasa na mitazamo au tafsiri ya uchumba kwa watu husika. Fahamu kwamba tafsiri unayokuwa nayo juu ya mchumba wako ndiyo inayokuongoza kujenga mahusiano ya aina fulani pamoja naye.
Lengo la somo hili ni;
Kuongeza ufahamu wa wachumba kuhusu kipindi hiki na Kuwapa vijana maarifa ya kuwasaidia kuishi kwa nidhamu ya Ki-Mungu katika uchumba wao. Pia ni kuwafikirisha vijana wanaotarajia kupita katika kipindi hiki mambo ya kuzingatia. Si wachumba wengi wanajua, Mungu anawataka wafanye nini katika uchumba wao au kwa lugha nyingine si wachumba wote wanaojua kwa nini kipindi cha uchumba kipo. Naam katika somo hili tumeandika mambo hayo kinaga ubaga.
Kwa kuwa suala la uchumba ni pana na lina mitazamo mingi, yafuatayo ni mambo tuliyozingatia katika uandishi wa somo hili;
  • Kuna makundi mbalimbali ambayo yana taratibu zao kuhusu mchakato wa mtu kumpata mke au mume kikiwepo kipindi cha uchumba. Makundi hayo ni pamoja na makanisa, makabila, familia nk.
  • Wachumba wanaweza kutofautiana kwa kiwango cha elimu, uchumi, ufahamu juu ya mambo mbalimbali, kikabila, umri na hata kwa rangi pia.
  • Kuna baadhi ya wachumba hadi kufikia muda wanakubaliana kwamba watakuja kuishi pamoja walishafahamiana tangu zamani na wengine hawakufahamiana.
  • Wachumba wanaweza wakatoka katika madhehebu/makanisa tofauti na hili ni kwa kuzingatia madhehebu/makanisa mengi yaliyopo.
Lengo letu ni kuandika juu ya mwongozo wa Neno la Mungu katika kipindi cha uchumba. kwa lugha nyingine, je Mungu anataka wachumba wafanye nini katika kipindi chao cha uchumba?. Kumbuka uchumba ni kipindi/wakati. Basi kama ni wakati jua kabisa kuna baadhi ya mambo ambayo ni lazima yafanyike, kwani Biblia inasema katika Mhubiri 8:5b “ Na moyo wa mwenye hekima hujua wakati na hukumu”, neno hukumu linamaanisha maamuzi, mambo ya kufanya.  
Yafuatayo ni mambo ya msingi kufanya katika kipindi cha uchumba;
Jambo la kwanza –  Mruhusu Roho Mtakatifu afanyike Bwana wa uchumba wenu
2Wakorinto 3:17 ‘Basi Bwana’ ndiye Roho; na alipo Roho wa Bwana, hapo ndipo penye uhuru’.
Kumbuka Roho Mtakatifu ni msaidizi. Hivyo basi ni vema kumtumia vema hasa katika nyanja hii ya mahusiano katika kipindi hiki cha uchumba. Ni Roho Mtakatifu pekee mwenye uwezo wa kukujulisha mambo na siri nyingi kuhusu mchumba wako hata kama yeye hataki kukueleza. Ukimruhusu Roho Mtakatifu afanyike Bwana, yeye atakuongoza katIka kufanya maombi yanayolenga maeneo ya msingi juu ya huyo mwenzako. Kila mtu ameumbwa pamoja na mapungufu fulani au kwa lugha nyingine mapungufu/ udhaifu (weakness) ni sehemu ya maisha ya mwanadamu. Roho Mtakatifu anapokuwa Bwana wa mahusiano yako yeye atakusaidia kuona madhaifu au mapungufu ya mwenzako kama kitu cha wewe kujivunia(Strength) kwa maana ya kuona udhaifu wa mwenzako kama kitu chema na si kibaya.
Kumbuka Paulo katika 2Wakorinto 12:9-10. —‘Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ….kwa hiyo napendezwa na udhaifu——- maana niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu. Hivyo Roho Mtakatifu atabadilisha tafsiri ndani yako za vyote unavyoona kwa mwenzako huenda juu ya umbile lake, umri wake, macho yake, kabila lake viwe vitu vya wewe kujivunia. Zaidi Roho Mtakatifu pia atakuongoza katika maombi yatakayosidia kuuondoa ule udhaifu ambao umekuja si katika mapenzi ya Mungu, yaani wa kishetani.
Jambo la pilini wakati wa kuweka msingi imara wa uchumba wenu na kufahamiana zaidi.
Hili jambo ni la muhimu  kuzingatia. Ni vema wachumba wakatafsiri na kuelewa vizuri maana ya uchumba. Wachumba wanapaswa kuwa na mipaka fulani katika uchumba wao na  kuwa makini kwa kujilinda na mazingira ya kila namna ambayo yanaweza yakapelekea wao kuanguka dhambini. Ni vema mkajua kwamba ninyi ni wachumba na si wanandoa. Na kama ni wachumba basi uchumba una mipaka yake na hamruhusiwi kufanya mambo ya wanandoa. Mipaka hii iwe kwa habari ya kutembeleana,kupeana zawadi, mawasiliano (ingawa mnapaswa kuwa makini na lugha mnazotumia pia) nk.  Lengo la kutafsiri misingi ya mahusiano yenu ni kujiwekea mipaka na mazingira yatakayowasaidia kuishi maisha ya nidhamu, ushuhuda na kumletea Mungu utukufu.
Sambamba na hili sehemu kubwa ya wachumba huwa wanakuwa hawafamiani vizuri. Japo wapo baadhi ambao walianza tangu shule za msingi/sekondari/chuo na sasa wamechumbiana hivyo kwa sehemu wanafahamiana vema. Kwa wale wasiofahamiana vema huu  ni wakati wa kumjua mwenzako vizuri kwa maana ya kabila lake, familia yake, umri wake, interest zake, matatizo aliyo nayo yeye binafsi au ya kifamilia, mitazamo yake juu ya mambo mbalimbali kama uchumba, ndoa, maisha, wokovu, neno la Mungu nk. Huu ni wakati wa kumjua mwenzako kwa njia ya maswali mbalimbali ya msingi yanayohusu vitu nilivyovitaja hapo juu. Lengo hapa ni kujua mapungufu/madhaifu(weakness) na mazuri(Strength) za mwenzako ili mjue namna ya kukabilana na mapungufu na namna ya kuendeleza yaliyo mazuri.
Ni vema pia kuulizana historia zenu za maisha ya nyuma. Kabla ya kuokoka umepitia katika mifumo gani ya maisha ambayo imechangia kukufanya uwe ulivyo. Kabla ya kumpata uliye mpata ulikuwa umefuatwa na wangapi na uliwakubalia au la, na kama uliwakubali kwa nini mliachana, na sasa wako wapi, je bado wanakufuatilia. Hii itawasaidia sana kujipanga vizuri kimaombi na katika mahusiano yenu na zaidi itawasaidia kuweza kuchukuliana na kuhifadhiana katika madhaifu ya kila mmoja.
Mungu anapowaunganisha anakuwa na kusudi maalum. Hivyo jua kwamba huyo mwenzi uliyepewa umepewa kwa ajili ya kusudi fulani la Mungu. Ni wachumba wachache sana ambao pindi wanapokutana kila mmoja anakuwa anajua walau kwa sehemu kwa nini aliumbwa. Sasa ni vema mkae chini mfikiri, nini Mungu anataka kukifanya duniani kupitia ninyi? Na zaidi angalieni kazi zenu au yale mnayoyasomea, Je mtawezaje kuliimarisha agano la Bwana kwa pamoja kama mke na mume?.
Hapa maana yetu mnatakiwa kujibu maswali yafuatayo? Je ni kwa nini mlizaliwa? Je kwa nini Mungu amekuunganisha na huyo uliye naye sasa? Na je kupitia elimu, bisahara zenu au kazi mlizonazo mtawezaje kuimarisha agano la Bwana?, Kwa kuzingatia vipawa na uwezo Mungu aliowapa, je ni wapi Mungu anataka kuwapeleka na kuwafikisha? Kama ndani yenu mna huduma fulani, je ni watu gani ambao Mungu atataka mshirikiane nao katika huduma hiyo?, je ipi ni nafasi yenu katika mwili wa Kristo na taifa kwa ujumla? Ni vema zaidi mwanaume akajua wito/ kusudi aliloitiwa ili pia amshirikishe na mwenzake.
Kufanikiwa kwa hili kunahitaji uwepo muda wa kutosha wa wachumba kukutana ili kupanga na kuweka mambo yao mbalimbali, na kama ni watu walioko mbali basi suala la mawasiliano kwa njia mbalimbali kama simu, barua pepe, na barua na hata zawadi ni la muhimu.
Jambo la tatu- ni wakati wa kulinda wazo la Mungu hadi litimie.
Siku zote uamuzi wowote unaoufanya una gharama. Naam uchumba pia una gharama nyingi Sana za kuzikabili kuliko unavyofikiri. Gharama hizo ni pamoja na muda, pesa, mawasiliano, maombi, uhuru nk. Kumpata mchumba au mwenzi ambaye ni wa kusudi la Mungu, usidhanie ndio umemaliza. Kama huo uchumba wenu ni wa mapenzi ya Mungu muwe na hakika mtakutana na vita kubwa sana katika kipindi hicho cha uchumba na lengo ni kuwatenganisha. Ni lazima mjifunze siku zote kuombeana kwa kumaanisha maana Shetani naye yupo kazini ili kuvuruga hayo mahusiano.
Kumbuka huyo mwenzi ni agano toka kwa Bwana hivyo unawajibika kumlinda, kumlinda ni pamoja na kuhakikisha wewe hausabibishi au haufanyiki chanzo cha ninyi wawili kuanguka dhambini, au ukamwacha na kumsababishia majeraha ya nafsini na hivyo kuharibu mahusiano yake na Mungu. Wapo watu waliofikia kuharibu mahusiano yao na Mungu kisa mchumba, saa ya ibada imefika mchumba anasema twende zetu out bwana, unataka kufanya maombi ya kufunga mchumba anasema kesho nitakutoa out, inagharimu sana muda wa kuwaza pia kwa ajili yake na familia yake au mahitaji mbalimbali aliyo nayo.
Zaidi pia uchumba unaweza kukunyima uhuru hata wa kuwa na maongezi na rafiki zako, maana kuna baadhi ya watu huwa hawataki kuona mchumba wake anaongea au kucheka na watu wengine, na pia kuna wengine ni wachumba lakini wamewekeana taratibu ngumu utafikiri wanandoa kabisa na ukweli zinawatesa ila kwa sababu hataki kumpoteza huyo mchumba wake inabidi avumilie.  Jambo tunalosisitiza hapa ni kwamba, uchumba una gharama nyingi angalia mahusiano yako na Mungu yasiharibikie hapa.
Jambo la nne- ni wakati wa kupanga malengo na mikakati yenu ya baadae.
Mithali 29:18a “Pasipo maono, watu huacha kujizuia’
Hili si jambo ambalo vijana wengi hulipa kipaumbele linavyostahili. Katika hili ni vema wachumba wafikirie mapema ni aina gani ya maisha ambayo wangependa kuwa nayo, na pia je ni aina gani ya ndoa wanataka kufunga, tatu je ni wapi wangependa kuja kuishi kwa maishayaoyote. Haya yatawasaidia wahusika kujipanga ndani na nje kukabiliana na yaliyo mbeleyao.Kamawanataka kufunga harusi kanisani basi maana yake wanahitaji kuwa na maandalizi mazuri kifedha, waweke katika muda kila wanalotaka kuelekea katika harusiyaoili iwasaidie kujiaadaa mapema. Malengo yoyote yale ambayo mtaweka basi hakikisheni yanatekelezeka, yanafikika, yanapimika na mnayapangia muda wa utekelezaji.
Mambo zaidi ya kuzingatia katika malengo yenu;
Katika hili ni vizuri wachumba waangalie nafasi yao kifedha imekaaje, na changamoto zinazowakabili wote kwa pamoja. Je hali yao kifedha inawaruhusu kuzikabili gharama za maandalizi ya ndoa kwa ujumla. Je hali ya kimaisha ya kijana wa kiume inamruhusu wakati wowote baada ya kuchumbia aweze kufunga harusi kama anataka. Je nafasi zao kielimu zikoje, je kama zinatofautiana ni kwa kiwango gani? Na je tofauti zao kiuchumi na kitaaluma zinaweza kuwa kikwazo kwao kuoana, au kwa wazazi wao nk. Na je baada ya kuwa wamegundua na kupima uwezo wao katika hayo mambo mawili, je wanaweza wakasaidianaje ili wafike mahali pazuri wote wawili.
Vijana wengi wa kiume huwa wanakosea sana hapa, wengi huwa wanasema sitaki kuchumbia/kuoa mpaka niwe nimesha jikamilisha kiuchumi, niwe angalau na maisha mazuri. Sisi hatushauri sana dhana hii, ukweli ni muhimu kwa kijana wa kiume akjikamilisha kwa yale mambo ya msingi. Lakini fahamu kwamba kuna wakati mwingine kuendelea kwako kiuchumi, au kuvuka kwako kimaisha ni rahisi zaidi pale unapokuwa na mchumba au ndoa yako. Tunasisitiza tena ni vema wachumba wakae chini na kufikiri ni kwa namna gani wataendelezana kiuchumi na kitaaluma. Angalizo, ni vema uwe na uhakika kweli huyo mtu ni wa mapenzi ya Mungu kwa maana ya kuwa ni wa kwako kweli, maana wapo wachumba ambao wamekuwa wakisaidiana mpaka kulipiana ada, kupeana mitaji, kununuliana nyumba, magari nk, halafu mwishowe mmoja anavunja maagano, maumivu yake ni makubwa sana.
Jambo la tano – ni wakati wa matengenezo na kuzijenga nafsi zenu
Wachumba wengi huwa wanafichana mambo mengi sana wanapokuwa wachumba na matokeo yake hawayashughulikii mapema na hivyo yanakuja kuwaletea shida kwenye ndoa. Huenda kabla hujakubaliwa wewe tayari mwenzako alikuwa amesha wakubali vijana au mabinti wengine kwamba ataolewa nao au kuwaoa. Pia  kama ni msichana huenda ameshawahi kubakwa, au kutokana na masumbufu ya kupata mtu sahihi na wakati mwingine kuachika mara kwa mara imefika mahali huyo msichana akasema sitaki kuja tena kuolewa. Zaidi  huenda  mmoja wenu huko nyuma ameshawahi kufanya uasherati au zinaa kabla hamjachumbiana. Au kuna mwingine amekuwa akisumbuliwa na tatizo la harufu, kufanya tendo la ndoa na mapepo nk.
Haya yote na mengine mengi yanayofanana na haya yana athari kubwa sana kiroho na kimwili kwenu kama wachumba na wanandoa watarajiwa kama hayatashughulikiwa vema katika kipindi hiki cha uchumba. Licha ya kuwa na athari mambo hayo yamepelekea nafsi za watu au wachumba wengi kujeruhika. Nafsi inapojeruhiwa inaharibu ndani ya mtu mfumo wa kufanya maamuzi, mfumo wa utiifu kwa Mungu wake, mfumo wa kunia na kuhisi pia. Sasa mifumo hii inapoharibika inapelekea watu kufanya maamuzi ambayo yapo nje ya mapenzi ya Mungu kabisa. Nawajua baadhi yao ambao wameacha na wokovu, na, wengine wamekata tamaa ya kuolewa, wapo walioamua kuolewa na mataifa ilimradi ameolewa nk.
Hivyo basi tumieni wakati huu kufanya matengenezo na kujengana nafsi zenu kwa maana ya kuombeana sana, pili kwa kuongeza ufahamu wenu katika neno  la Kristo hasa maandiko yanayolenga uponyaji katika nafsi zenu, tatu kufuta na kufisha mapatano/maagano yote ambayo mmoja wenu aliyafanya huko nyuma na watu wengine na pia kufuta picha za kubakwa na kujenga ufahamu wa mtu aliyeathirika kisaikolojia kutokana na mambo kama hayo kwa njia ya Damu ya Yesu. Hatua hizi zitawasaidia kurejesha mifumo iliyoharibika na kuziruhusu nafsi zenu zifanye kazi kama inavyotakiwa.
Jambo la sita – ni wakati wa kujua taratibu mbalimbali kuelekea kwenye ndoa
Tumeshasema, kila dhehebu au kabila wana taratibu zao kuhusu uchumba hadi ndoa. Hivyo ni vema wachumba, wakafuata taratibu ambazo zimewekwa na makanisa yao hasa zile ambazo zipo katika mapenzi ya Mungu. Lakini pia lazima tukubali kwamba kuna baadhi ya taratibu za makanisa, makabila na hata madhehebu ambazo nyingine zipo tu lakini hazitekelezeki na nyingine hazimpendezi Mungu.
Sasa ni vema wachumba wazijue hizo taratibu na wajue je wanaweza kuzitekeleza au la, na kama hawawezi wafikirie kabisa wanafanyeje. Mfano kuna baadhi ya makanisa ambayo hayaruhusu mtu wa kwao aoe au kuolewa na mtu wa nje ya dhehebu hilo. Sasa hii ina maana kama una mchumba wa aina hiyo jipange kujibu maswali ya wazee wa kanisa na Mchungaji vizuri. Na zaidi kuna baadhi ya makabila na familia hazitaki uoe au kuolewa na watu nje ya kabila lako, au aliyekuzidi umri kama wewe ni kijana wa kiume nk. Hivyo ni vema kuzijua hizo taratibu ili mjue mnajipangaje kukabiliana nazo. Ushauri wetu ni huu kama una uhakika huyo mtu ni wa kutoka kwa Mungu basi simamia la Bwana maana lipi jema, kumpendeza Mungu au wanadamu?. Kumbuka Mungu ndiye mwenye ratiba ya kila mmoja wetu.
Suala la  kukagua/kupima afya zenu kwa pamoja.
Kwa mazingira ya ulimwengu wa sasa suala la ukimwi limechukua sura mpya na kuleta mtafaruku ndani ya kanisa hasa kwa vijana wanochumbia kabla ya kupima afya zao. Siku hizi jambo hili limewafanya wachungaji kuomba sana kwa habari ya vijana ndani ya kanisa. Sasa kama mlikuwa hamjapima afya zenu mpaka mmechumbiana basi chukueni hatua mwende kupima. Ni vema wachumba wakapima mapema afya zao ili jambo hili lisije likawaletea shida baadaye, maana kwa sheria ya nchi yetu wachungaji hawaruhusiwi kufungisha ndoa kama mmoja wa wahusika ameathirika.
Upimaji wa afya zenu ni wa muhimu kwani, ndani ya makanisa kuna rekodi ya vijana wengi tu ambao wameshaathirika na huenda si kwa sababu ya zinaa, maana kwa mujibu wa watu wa afya njia za maambukizi ni nyingi. Kuna wengine wamezaliwa nao, kwa nia ya kuongezewa damu,kutumia vifaa kama nyembe, sindano nk. Hata hivyo swali la msingi inabaki kwamba je, liko tumaini kwa mtu aliyeathirika kuoa au kuolewa?  
Tukueleze hivi, hakuna jambo gumu lolote la kumshinda Bwana, hii ni pamoja na ukimwi, kama Mungu alimfufua Lazaro, alitenganisha bahari ya Shamu na watu wakapita, kama Yesu alitembea juu ya maji, basi naomba ujue kwamba Ukimwi hauwezi kuzuia kusudi la Mungu hapa duniani kwa wale awapendao na kwa sababu hiyo tunasema hata kama mtu ana ukimwi na Mungu bado ana kazi naye hapa duniani, hakika atamponya huo ukimwi na atampa mke au mme.
Faida na lengo la kupima ni hili, hata kama majibu yatatoka mmoja ameathirika isiwe mwanzo wa ninyi kuachana. Kama mna uhakika Mungu aliwaanganisha huu ndio wakati wa kurudi mbele za Mungu kwa maombi ya uponyaji na kujipanga zaidi juu ya hilo.
Jambo la saba – ni wakati wa kuongeza ufahamu wenu kuhusu nafasi yako kwenye ndoa.
Je umeshawahi kujiuliza ni kwa nini Mungu anakupa mke au mme? Yamkini zipo sababu nyingi lakini baadhi yake ni; Mungu anakupa mke kama msaidizi, mlinzi, na pia unapopata mke au mme unakuwa umejipatia kibali kwa Bwana na pia ni kwa sababu ya zinaa ndio maana unahitaji mwenzi. Hizi ni baadhi ya sababu zilizoko ndani ya Biblia. Hivyo basi tafuteni wanandoa mnaowaamini na zaidi waliokoka  muwaulize   kuhusu wajibu  wa kila mmoja kwa nafasi yake kwenye ndoa. Katika hili baadhi ya makanisa  huwa yana utaratibu wake wa nani atahusika na maelekezo ya aina hii kwa wachumba. Hivyo kama kanisa lako lina utaratibu huo, fuata huo utaratibu.
Katika ndoa kuna mambo mengi sana ambayo mtatakiwa kufanya, ni vema kufuata mwongozo na ushauri wa viongozi wenu au wachungaji wenu kuhusu nini mnatakiwa kufanya katika ndoa yenu. Angalizo hapa ni hili, uwe makini na vyanzo vya ushauri au mafunzo katika eneo hili ili lisije kuleta madhara baadae. Usitafute wala kufuata kila ushauri, bali sikiliza pia uongozi wa Mungu ndani yako.
Jambo la nane– Msifanye tendo la ndoa, maana jambo hili litaharibu mpango wa Mungu na kusudi lake kupitia ninyi.
Wakati wa uchumba, si wa kufanya mapenzi au kufanya michezo ya mapenzi. Tunarudia tena ili kuonyesha msisitizo kwamba chonde chonde jamani, uchumba sio ndoa, maana uchumba unaweza kuvunjika. Hairusiwi kabisa kwa wachumba kufanya mapenzi kwa maana ya tendo la ndoa kabla ya ndoa. Kitendo cha Mungu kukujulisha/kukupa huyo mwenzako kama mke/mume mtarajiwa haina maana mna haki ya kufanya mambo ya wanandoa. Mungu kukupa huyo mwenzako sasa ni taarifa kwamba  huyu ndugu ndiyo atakuwa mkeo au mmeo na anakupa taarifa sasa ili ujipange kufanya mambo ya msingi mnayotakiwa kuyafanya katika kipindi cha uchumba. Kipindi cha uchumba ndicho kipindi ambacho wachumba wengi sana wanavuruga kusudi la Mungu, na kuharibu maisha yao ya baadae na ndoa yao kwa ujumla.
Ndoa nyingi sasa hivi zina migogoro kwa sababu wakati wa uchumba walidiriki kufanya tendo la ndoa. Vijana wengi hawajajua kufanya tendo la ndoa kipindi cha uchumba lina madhara gani kwao na ndio maana wengine wanafanya. Biblia inasema katika Mithali 6:32 “Aziniye na mwanamke hana akili kabisa, afanya jambo litakalomwangamiza nafsi yake mwenyewe”. Hata kama ukifanya tendo la ndoa na mchumba wako ambaye mlibakiza siku moja kufunga harusi, bado umezini.
Ndani ya nafsi ya mtu kuna akili, hisia, nia na maamuzi. Biblia inaposema afanya jambo litakalomwangamiza nafsi yake ana maana hii, dhambi hii inapofanywa, ina haribu mfumo wa utiifu na uamnifu kwa Mungu wako, inapelekea kukosa usikivu wa rohoni kabisa, ina haribu mfumo wa kufikiri, kunia na kufanya maamuzi. Na kwa sababu hiyo si rahisi tena kusikia na kutii uongozi wa Roho Mtakatifu. Kwa watu ambao wamezoea kuwa na mahusiano mazuri  na Mungu watanielewa ninachosema hapa.
Zaidi kuna baadhi ya wachumba kweli hawafanyi tendo la ndoa bali wanafanya michezo ya mapenzi. Michezo ya mapenzi (Fore play) ni maalum kwa ajili ya wanandoa, na ni sehemu ya tendo la ndoa. Hivyo kufanya michezo ya mapenzi ni kufanya mapenzi kwa sababu ile ni sehemu ya mapenzi. Kuna vitu unavichochea,  unaamusha hamu ya mapenzi au unayachochea mapenzi. Biblia inasema katika Mhubiri 2:7 “Nawasihi, enyi binti za Yerusalemu, kwa paa na kwa ayala  wa porini, msiyachochee mapenzi, wala kuyaamsha, hata yatakapoona vema yenyewe.”
Mungu pia anachukia michezo ya mapenzi soma Isaya 57:4-5 “Mnafanya dhihaka yenu juu ya nani, juu ya nani mmepanua vinywa vyenu, Na kutoa ndimi zenu? Je, ninyi si wana wa uasi, uzao wa uongo; ninyi mnaowasha tamaa zenu kati ya mialoni, chini ya kila mti wenye majani mabichi….. Wachumba wengi hawajui haya kwa sababu si makanisa yote yanayofundisha maswala ya mahusiano ya wachumba kimpana.
Mpaka hapa tunaamini umeshajua hasara za jambo hili  na utazijizuia kabisa kulifanya. Michezo ya mapenzi ni pamoja na kunyonyana ndimi, kushikana sehemu ambazo zinaamsha ashiki ya mapenzi kama sehemu za siri, matiti, kiuno nk, pamoja na kuangalia picha za ngono. Katika kipindi ambacho tumemtumikia Mungu kupitia vijana tumejifunza na kukutana na kesi mbalimbali za aina hii na kuona namna Shetani anavyovuruga mpango wa Mungu kwa vijana. Mwenye sikio na asikie neno ambalo Roho wa Bwana awaambia vijana ili kulida kusudi la ndoa.
Ni imani yetu kwamba mambo haya nane yameongeza ufahamu na hivyo kuwa maarifa ya kutosha kukusaidia kuenenda kwa mapenzi ya Mungu katika kipindi cha uchumba.
Bwana awabariki

JIFUNZE KUFIKIRI KABLA HUJACHUKUA UAMUZI WA KUOA AU KUOLEWA

Nawasalimu kwa jina la Yesu . Leo katika nyanja hii ya vijana, nimeona ni vema tukashirikishana kuhusu suala la ‘kufikiri kabla ya kuoa au kuolewa’.
Siku moja katika kusoma Biblia nilikutana na mstari ufuatao, nakushahuri uusome kwa umakini. Biblia katika 1Wakorinto 7:8-9 inasema “Lakini nawaambia wale, wasiooa bado na wajane, Ni heri wakae kama mimi nilivyo, lakini ikiwa hawawezi kujizuia, na waoe, maana ni afadhali kuoa kuliko kuwaka tamaa”.
Baada ya kuusoma mstari huu niliingia katika tafakuri nzito sana ambayo mwishowe ilinipeleka kuandaa somo hili, kwamba ni vema ukafikiri vizuri kabla ya kuchuka uamuzi wa kuoa au kuolewa.
Unajua malezi, dini, madhehebu yetu, wazazi, mila na desturi vinachangia kwa kiwango kikubwa sana kuhusu utaratibu wa kuanzia mtu kupata mke au mume mpaka watakapofunga ndoa. Kila kundi lina mfumo na utaratibu wake ambao lingependa vijana waufuate ili kuhakikisha wanaoa na kuolewa kwa kile ambacho kila kundi linaona na kuamini kwamba huo ndio uataratibu mzuri kufuatwa.
Namshukuru Mungu kwa kuwa nami nimeoa, ingawa vitu vingi sana Bwana alikuwa ananifundisha vinavyohusu ndoa hata kabla sijaoa. Nakubaliana na dhana kwamba ili uweze kuwa Mwalimu mzuri kwenye nyanja fulani basi ni lazima au ni vema wewe mwenyewe ukawa umepitia kwanza kwenye nyanja hiyo. Lengo ikiwa sio tu ufundishe ‘theory’ bali pia utufundishe na uzoefu wako binafsi kwenye eneo hilo. Licha ya kukubaliana na dhana hii, kwangu binafsi haikuwa hivyo, maana kuna mambo mengi ambayo, Bwana Yesu, alikuwa ananifundisha yanayohusu ndoa hata kabla sijaoa.
Kwa kifupi ndoa ni shule au darasa ambalo wanandoa wanatakiwa kukaa chini na kujifunza kila siku namna ya kuishi humo ndani ili kuweza kuishi maisha ambayo Mungu amewakusudia.
Kutokana na mifumo ya baadhi ya makanisa yetu, si vijana wengi ambao wanafundishwa kwa undani kuhusu maamuzi haya makubwa. Wengi wao wameingia kimwili na kujikuta wakijutia na kulaumu kwa nini nilimuoa au kuolewa na huyu kijana. Nasema haya kwa kuwa nimekutana na wanandoa wengi wa aina hii, na nataka nikuambie kama Biblia ingetoa mwanya wa wanandoa kuachana na kuoa au kuolewa na mtu mwingine, wapendwa wengi sana walioko kwenye ndoa wangefanya hivyo na wengine wasingekubali kuolewa au kuoa tena.
Unajua kwa nini?
Ni kwa sababu si vijana wengi wenye ufahamu wa kutosha juu ya aina ya maamuzi wanayotaka kuyachukua. Kwa hiyo katika somo hili nimeona vema niandike mambo manne ya msingi ambayo naamini yataongeza na kupanua ufahamu wako ili kukusaidia kufikiri kwanza kabla ya kufanya maamuzi haya makubwa;
  • Si kila ndoa inayofungwa imeunganishwa na Mungu, kwa kuwa ndoa ni kiungo cha muhimu kwa Mungu na Shetani pia.
Kuanzia mwaka 2005, Mungu alinipa kibali cha kuanza kufundisha na pia kushauri  juu ya mambo kadhaa kuhusu wanandoa. Tangu wakati huo hadi sasa nimekutana na baadhi ya wanandoa ambao wanajuta kwa nini walikubali kuoa au kuolewa. Wanaishi kwenye ndoa kwa sababu tu ya watoto na pia kwa hofu kwamba endapo kama wataachana jamii na watu wanaowazunguka hawatawaelewa.
Ni vizuri ukafahamu kwamba si kila ndoa inayofungwa ni ya mapenzi ya Mungu, hata kama imefungwa kanisani. Biblia inaposema kilichounganishwa na Mungu, mwanadamu asikitenganishe, katika nafasi ya kwanza maana yake iwe ndoa ambayo Mungu ndiyo aliyehusika katika kuanzisha mahusiano na kuwaongoza hao watu kuishi pamoja. Wakati Mungu anatafuta kuhakikisha watu wake wanaoana katika mapenzi yake na Shetani naye anapambana kuhakikisha watu wanaoana katika hila (mapenzi) zake.
Shetani amefanikiwa kwa kiwango kikubwa sana kuvuruga wanandoa wengi na kuwafanya waishi maisha tofauti na yale ambayo Mungu aliwakusudia. Ni kwa sababu hii ndio maana Paulo aliwaambia Wakorinto ‘Lakini nawaambia wale, wasiooa bado na wajane, Ni heri wakae kama mimi nilivyo, lakini ikiwa hawawezi kujizuia, na waoe, maana ni afadhali kuoa kuliko kuwaka tamaa’. Paulo aliona shida, maudhi ya wandugu walioko kwenye ndoa tokana na migogoro aliyokuwa akikutana nayo.
Fahamu kwamba ni furaha kubwa kwenye ufalme wa giza mtu anapooa au kuolewa kinyume cha mapenzi ya Mungu. Hii ni kwa sababu Shetani anajua akifanikiwa kukushawishi ukaoa kinyume na mapenzi ya Mungu, ameharibu ‘future’ yako na kile ambacho Mungu alikusudia ukifanye hapa duniani. Kumbuka suala sio kuoa au kuolewa tu, bali ni kuingia kwenye ndoa ambayo itakuwezesha kulitumika shauri la Bwana katika kizazi chako. Hivyo kabla hujaamua nani uishi naye hakikisha unamshirikisha Mungu akuongoze kumpata mwenzi sahihi.
  • Unapaswa kuoa au kulewa katika mapenzi ya Mungu
Naam kuoa au kuolewa katika mapenzi ya Mungu ni changamoto nyingine kubwa kwa vijana wa kizazi cha leo. Naam hili ni eneo ambalo Mungu yupo makini sana kufuatilia nani atakuwa mwenzi wako wa maisha. Na upande wa pili nao, Shetani anapigana kwa juhudi kubwa ili kuvuruga kusudi la Mungu kupitia mtu au watu.
Ni vizuri ukafahamu kwamba unapotaka kufanya maamuzi ya kutaka kuoa au kuolewa, Shetani naye ataleta mawazo (mapenzi) yake ndani yako juu ya nani anafaa zaidi  kuwa mwenzi wako maisha. Lengo lake ni kuhakikisha anakuunganisha na mtu ambaye anajua kwa huyo atakumaliza kiroho na kihuduma kabisa. Suala sio kuwazuia msiende kanisani, bali ni kuhakikisha kile ambacho ungefanya kwa kuwa na mtu sahihi hakifanikiwi. Ukitaka kujua ukweli wa jambo hili, muulize Mchungaji wako, kesi nyingi anazokutana nazo kanisani kwake zinahusu nini, naamini atakujibu kimapana. Ni jukumu lako kuwa makini kufuatilia unatii wazo la nani, Mungu au Shetani? 
  • Vigezo vya kimwili ni silaha kubwa ya uharibifu
Vigezo vya kimwili ni moja ya silaha kubwa ambazo Shetani anazitumia kuwavuruga watu wengi waweze kuoa au kuolewa nje ya mapenzi ya Mungu kwao. Jifunze kufukiri na kutafsiri mambo au makusudi kama Mungu anavyotazama na kutafsiri. Na uwezo wa kufanya hili utaupata kwenye neno lake tu. Kwako mwanaume Mungu anapokupa mke anakupa Mlinzi na msaidizi. Na kwa mwanamke Mungu anakuwa amekupa kichwa. Ni muhimu sana kuchunga ni msaidizi, mlinzi au kichwa gani unataka kiunganishwe na maisha yako kwa njia ya ndoa.
  • Ndoa ni wajibu mkubwa
Ndani ya ndoa kuna wajibu mkubwa sana unaokusubiri kama baba au mama. Ndani ya ndoa muda na uhuru wako unabanwa na mwenzi wako. Ndoa inabana pia muda wa kuwa na Mungu wako. Na kwa wengi kwa kutaka kuwapendeza zaidi waume au wake zao, wamefarakana na Mungu, kwa sababu wamewapa waume au wake zao hata nafasi na muda wa Mungu kwenye maisha yao.
Usiingie ndani ya ndoa kwa fikra za uapnde mmoja. Naam ndoa ni wito wa mapungufu na uvumilivu ambao ni lazima uwe tayari kuchukuliana na mwenzi wako katika mapungufu yake. Kuna vitu hamtaweza kufanana na kwa sababu ya mapungufu yaliyopo kwa kila mmoja  unapaswa kutafakari kuhusu majukumu yanayokuja kwako kama mwanandoa, hekima na busara katika kuzikabili changamoto za ndoa, kama vile kuzaa au kutokuzaa, kutokujiweza katika masuala ya unyumba, matumizi ya fedha, tabia za mwenzi wako nk.
Haya ni mambo ya kuhakikisha unayaombea mapema ili kujenga msingi imara utakapoingia kwenye ndoa yako. Lakini nikutie moyo kwamba endapo utaoa au kuolewa katika mapenzi ya Mungu, yeye ni mwaminifu, atakuunganisha na mtu ambaye katika changamoto mtakazokutana nazo hazitawakwamisha wala kuwafanya mjute. Bali endapo Shetani ndiye ataongoza maamuzi yako, ni majuto makubwa sana (asomaye na afahamu).
Mungu akubariki, naamini ujumbe huu umeongezea mambo ya kutafakari na kuzingatia kabla ya kufanya uamuzi wa kuoa au kuolewa.

KIJANA ZINGATIA HILI, ILI UWEZE KULITUMIKIA KUSUDI LA MUNGU. “Huu ni waraka maalumu kwa vijana wote ambao bado hawajaoa au kuolewa”.


Kijana mwenzangu ninakusalimu kwa jina la Bwana. Katika mwezi huu nina neno fupi ambalo nimeona ni vema nikushirikishe na wewe juu ya ‘UMUHIMU WA KUUTAFAKARI MWISHO WAKO UKIUHUSIANISHA NA KUSUDI LA MUNGU JUU YAKO’

Tarehe 26/04/2012 nilifanya maombi maaulumu yaliyolenga kuombea vijana ambao bado hawajaoa au kuolewa, nikimsihi Mungu afungue milango ya wao kuoa au kuolewa, kwa sababu wengi wao ninaowasiliana nao bado hawajaoa au kuolewa.

Katika kunijibu Mungu alinipa mistari kadhaa na kunifunulia tafsiri yake, nami nikaandika kwenye kumbukumbu zangu na mwezi huu nimeona ni vema na wewe nikushirikishe mafunuo haya maana naamini yatakusaidia;   

Fungu la kwanza ni, Luka 19:41 – 44.
Soma fungu hili lote, mimi nitanukuu maneno machache tu. “Alipofika karibu aliuona mji, akaulilia, akasema, laiti ungalijua hata wewe, katika siku hii, yapasayo amani … siku zitakuja adui zako watakujengea boma … watakuangusha chini wewe na watoto wako … kwa sababu hukutambua  majira ya kujiwa kwako.

Fungu la pili ni, Isaya 1:2-3
“Sikieni enyi mbingu tega sikio ee nchi … kwa maana Bwana amenena; nimewalisha watoto na kuwalea nao  wameniasi, ng’ombe amjua Bwana wake, punda ajua kibanda cha Bwana wake, bali Israel hajui, watu wangu hawafikiri”.

Fungu la tatu (3) ni , Kumbukumbu  la Torati 39:29.
 “Laiti wangalikuwa na akili hata wakafahamu haya, ili watafakari mwisho wao”.

Katika mafungu haya matatu ya maandiko Roho mtakatifu alinifunulia yafuatayo;

*Kwanza alisema, usifikiri hao watu unaowaombea siwajibu. Wengi nilishawajibu, lakini wengine kwa sababu zao binafsi, wazazi wao, Viongozi wao n.k  hawajatii wazo langu juu yao/mapenzi yangu juu yao. Mimi ni Mungu ninayeangalia kesho/mwisho wa mtu/watu na lolote ninalofanya nimeliona mwisho wake. Sasa kwa kuwa hawa vijana wamekataa wazo langu kwa kutofikiria mwisho wao na kusudi langu kupitia wao na ndoa zao,  basi, hakika ndoa zao   zitakuwa na shida na baadhi yao wataniacha kabisa.

*Pili, Mungu kwa uchungu sana anataka mbingu na nchi zisikie na zijue kwamba   watoto wake ambao amewalisha na kulea  wamemuasi. Watoto hao wameshindwa kujifunza kupitia ng’ombe na punda, na tatizo lao ni kutokufikiri. Hii ina maana kutokufikiri kwao kumepelekea wao washindwe kumjua Mungu.  Kinamuuma sana Mungu, anapoona watu aliowaokoa na kuwafundisha au kuwaonyesha njia wapasayo kuiendea   wanakataa kwenda katika njia yake.

Zaburi 32:8 anasema “Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea, nitakushauri jicho langu likikutazama”. Sasa kitu kinachomuumiza ni pale anapowaonyesha watu njia yake au mapenzi yake kwao kuhusu wake/waume zao watarajiwa na akina nani halafu wao wanashindwa kutii. Licha ya kuwaonyesha au kuwajulisha mapenzi yake bado wameasi.


Ndugu kijana mwenzangu, natamani Mungu alete kitu hiki ndani yako kwa uzito ule ule aliouleta ndani yangu, ili usije ukakataa wazo la Mungu kwako na ukamkosea hata kuikosa mbingu kwa sababu tu ya mke au mume.

Sasa fanya yafuatayo ili kukaa katika mapenzi yake;

(a)   Jifunze kutafakari mwisho wako, ukijua ya kwamba mwisho wako uko mikononi mwa Mungu. Na kwa sababu hiyo maamuzi yoyote unayoyafanya ni lazima,  na si ombi umruhusu Mungu akuongoze ili uenende katika njia zake.
(b)   Haijalishi kwa jinsi ya mwili huyo mtu ana upugnufu/udhaifu wa aina gani kwa mtazamo wako, maadam una uhakika ni mtu wa mapenzi ya Mungu uishi naye, basi usijaribu kukataa huyo mtu kwa sababu Mungu ameona unakokwenda kukoje na huyo aliyemleta ndiye ambaye mtafika naye mwisho wenu.  
(c)    Hivyo basi wazo lolote/kijana/mtu yoyote anapokuja kwako kutaka   muoane na ndani yako unaona hakika ni mtu wa mapenzi ya Mungu, basi  kabla hujakataa kwa sababu zako binafsi, kaa chini utafakari, mhoji Mungu kwa maswali yanayokutatiza. Unapokwenda mbele za Mungu siku zote yeye ni mwaminifu atakupa majibu ya msingi na nina kuhakikishia unapotii uongozi wa Mungu kuna baraka za ajabu sana. Lakini unaposhindwa kutii  itakugharimu kuliko unavyofikiri.

  *Mungu anapokuonyesha/anapokupa mke au mme hamleti kwako kwa lengo la kukukomoa, bali anakua ameangalia kwanza kusudi lake, changamoto zilizopo mbele yenu na umbali mnaotakiwa kusafiri kwa pamoja kisha ndio anawaunganisha kwa kukupa mtu (mke au mume) ambaye anajua ukiwa naye hakika kusudi lake litafikiwa na mtaweza kuzikabili na kuzishinda changamoto zote zitakazojitokeza.

Hivyo mwenzi yoyote unayempata kama una hakika katoka kwa Mungu hata kama ana mapungufu gani kwa fikra zako au wazazi au dhehebu lako mimi nakushauri usimkatae, kwa sababu kwa huyo wewe utaweza kulitumikia shauri la Bwana.

Aliye na masikio na asikie lile ambalo Roho wa Bwana asema na vijana

KWA NINI ULIZALIWA AU KUUMBWA?

Mwanzo: 1:26“Mungu akasema, Na tufanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu, WAKATAWALE samaki wa baharini na ndege wa angani, na wanyama, na nchi yote pia na kila chenye kutambaa kitambaacho juu ya nchi”
Katika waraka huu nataka tujifunze juu ya kusudi la wewe kuumbwa na nini ufanye ili uweze kutawala.    Zipo sababu nyingi za wewe kuumbwa lakini moja wapo na kubwa ni ili wewe uweze kutawala. Dhana ya  utawala ni pana, mimi nimeigawanya katika nyanja za kiroho, kidini, kisiasa, kiuchumi, ki-ardhi, kibiashara, ki-taaluma nk.
Sasa aina ya utawala ninayotaka kuzungumza ni utawala katika nyanja ya siasa inayopelekea utawala katika serikali. Yafuatayo ni mambo ya msingi ambayo yatakusaidia wewe uweze kutawala sawasawa na kusudi la Mungu la kukuumba;
(a)Kwanza amini kwamba wewe unaweza kuwa kiongozi mzuri na pia siku moja utakuja kuwa kiongozi mzuri  katika serikali ya nchi yako. Amini kwamba hauna upako wa kupiga kura tu, bali pia tayari Mungu ameshakupaka mafuta (upako) wa kupigiwa kura na wakati ukifika wapiga kura watathibitisha hilo.
(b) Pili, amini kwamba inawezekana kabisa kuokoka na wakati huohuo ukawa mwanasiasa na kiongozi mzuri wa taifa lako. Jifunze kutoka kwa wafalme mbalimbali katika Biblia kama vile Daudi, Yehoshfati nk. Siasa sio mchezo mchafu kama wengi wanavyofikiri, shida ipo kwa wale waliojiingiza kwenye siasa. Kama wanasiasa unawaona kama hawafai kwa kuwa ni waongo, au wala rushwa haina maana siasa ni mbaya.
(c)Fanya maamuzi ya kujiunga na chama chochote chenye sera nzuri katika nyanja zote za msingi na hasa kiuchumi. Nakushauri kabla hujajiunga na chama chochote, soma kwanza sera zao, uzielewe na kuzipima vizuri na kisha sasa amua kujiunga na chama hicho baada ya kuwa umeridhika na kuamini kwamba unaweza fanya nao kazi.
(d)Gombea kila aina ya uongozi katika chama chako kwa nafasi zake mbalimbali.
Kuanzia chini mpaka nafasi ya juu. Chukua fomu za uongozi, jaza bila kuwa na shaka, mwombe  Mungu akufanikishe, usiogope kushindwa katika uchaguzi, hayo ni matokeo na haina maana kwamba haufai, huenda sio wakati wa Bwana lakini pia kama kuna makosa uliyofanya jirekebishe
(e)Jenga mahusiano mazuri na makundi mengine katika jamii.
 Usiwabague watu kwa rangi, umri, kabila wala dini zao. Maana hao watu kwanza ndio utakaowaongoza ukipita, wao ndio watakaokupigia kura na zaidi baadhi
yao utafanya nao kazi katika ofisi moja.
(f)Mwisho ongeza ufahamu na Imani yako kuhusu siasa/uongozi. Nenda kwenye Biblia soma mistari yote inayohusu mambo ya utawala na uongozi ili uongozeke kiimani na pia zaidi ya hapo pia ongeza elimu ya dunia hii kuhusu mambo ya siasa.
Naamini ujumbe huu mfupi utakubadilisha kufikiri kwako kuhusu utawala (siasa) na kisha utayafuatilia mambo ya uongozi kwa karibu, hii ikiwa ni pamoja na kujiunga na chama chochote cha kisiasa hapa nchini.

KWA NINI TATIZO LA FEDHA LIMEKUWA SEHEMU YA MAISHA YA WAKRISTO?




Biblia imeshaweka wazi katika Yerema 29:11 na 3 yohana 1:2 kwamba mawazo aliyonayo Mungu juu yetu ni mawazo/mipango ya kutufanikisha, si hivyo tu bali anataka tufanikiwe katika mambo yote. Pia tunajua kwamba fedha na dhahabu ni mali ya Bwana si hivyo tu bali sehemu kubwa ya Biblia imejaa ahadi za Mungu za kutufanikisha kifedha na mafundisho mengi ya pesa.
Sasa licha ya haya yote na ukweli kwamba tumemwamini huyu Yesu lakini bado maisha ya mkristo mmoja mmoja, wakristo wengi, kanisa kwa ujumla, kwaya, makundi ya kiroho na huduma mbalimbali hali yake ya kifedha ni ngumu. Kila mtu analalamika juu ya pesa, mpaka imefika mahali tatizo la fedha limekuwa sehemu ya maisha.
Mikutano, semina tumeshindwa kufanya kisa fedha, vijana wameshindwa kuoa kisa pesa, kwaya hazirekodi kisa fedha. Kitu gani kimetokea kwa wakristo. Wazungu wanasema “Something must be wrong some where” maana yake lazima kuna kitu hakijakaa sawasawa mahali fulani.
Kusudi la waraka huu mfupi ni kukuelezea sababu ambazo zimepelekea tatizo la fedha kuwa sugu na kwa sehemu ya maisha kwa wakristo wengi. Sababu hizo ni ;
Moja, kukosa maarifa (mafundisho) ya kutumia fedha ki-Mungu. Hosea 4:6a Fedha ina kanuni zake za matumizi. Hivyo kushindwa kujua kanuni hizo na namna ya kuzitumia hizo fedha ki-mungu basi tatizo litaendelea kuwapo.
Mbili, matumizi ya fedha ya Mungu nje ya kusudi lake.
Hagai 2:8, Sikiliza fedha ni mali ya Bwana, hata ikiwa mikononi mwako bado ni ya Bwana, hivyo ni lazima itumike kwa mapenzi yake, maana kila pesa anayokupa ndani ina kusudi fulani au anakupa kwa lengo fulani.
Tatu, Roho ya mpinga kristo inafanya kazi ndani ya fedha.
 2 wathesalonike 2:7, sikiliza, shetani anajua ukiwa na fedha yeye atakuwa na hali ngumu sana maana utaituma hiyo fedha kuimarisha agano la Bwana, hivyo ameweka Roho ya mpinga kristo ndani ya fedha ila kupinga  fedha isiende kwa watu wa Mungu ili washindwe kumtumikia Mungu.
Nne, kukosa nidhamu katika matumizi ya fedha.
Tito 3:14 Watu wengi hasa waliokoka, hawana nidhamu katika matumizi ya fedha pindi inapofika katika mikono yao. Hawana malengo mazuri katika mtumizi ya fedha na kwa sababu hiyo wanajikuta fedha wanayoipata inatumika kienyeji na kwa sababu hiyo tatizo la fedha lina baki palepale.
Tano,Ufahamu mdogo wa Neno la Mungu kuhusu fedha.
 Wakristo wengi sana wanayo mistari mingi sana inayozungumza uponyaji na kutoa mapepo, na hata imani yao imeongezeka kwenye maeneo hayo. Lakini kwenye eneo la pesa ufahamu wao ni mdogo sana, si wengi wanaopata mafundisho katika nyanja ya fedha ya kutosha.
Sita, Kuwategemea wanadamu na si Mungu .Katika Yeremia 17:5 Mungu ametoa ole kwa wale wanaowategemea wanadamu.Hii pia imekuwa sababu kubwa sana ya tatizo la pesa kuwa sugu. Ni kweli watu wanamuomba Mungu awabariki, lakini mioyo yao inawategemea wanadamu na tayari ole imeshatiliwa kwa mtu anayemtegemea mwanadamu ki-mafanikio.
Mwisho, ni vifungo na laana za kifamilia, kiuokoo, kitaifa nk.
 Kwenye eneo la pesa, kuna baadhi ya watu wamefungwa wasifanikiwe kifedha katika ulimwengu wa kiroho. Hili ni tatizo la kiroho zaidi na pia wengine ni laana zinazotokana na kushindwa kulijua neno la Mungu. Soma kumbukumbu 28:15-60.
Ni maombi yangu kwamba Mungu akusaidie kuwa na mahusiano mazuri na yeye hasa kwenye eneo la fedha ili uone baraka zake

KWA NINI MUNGU ANATAKA WATU WAKE WAWE MATAJIRI?

Ile mwanzo 12:2 neno inasema “nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki, na kulikuza jina lako, nawe uwe baraka”. Na Mwanzo 13:2 inasema“Naye Abramu alikuwa ni tajiri  kwa mifugo, na kwa dhahabu”.
Hapa tunaona jinsi Mungu anavyoweka ahadi ya kumbariki Abramu na kumfanya kuwa taifa kubwa. Kwenye sura ya 13 tunaona tayari Mungu ameshaanza kumbariki inasema alikuwa tajiri kwa mifugo, kwa fedha, na kwa dhahabu. Bado katika 3Yohana 1:2 Mungu anasema “mpenzi naomba ufanikiwe katika mambo yote na kuwa na afya yako, kama vile roho yako ifanikiwavyo .
Mpaka hapa tunaona kabisa ni mpango wa Mungu kutufanikisha katika mambo yote, hii ni pamoja na mafanikio ya kifedha. Na utajiri ambao Mungu anataka tuwe nao sio utajiri mdogo .
Sasa swali ni kwamba kwa nini Mungu anataka tuwe matajiri? Maana kuwa tajiri bila kujua sababu za kuwa na huo utajiri utashindwa kujizuia kwenye matumizi mabovu ya huo utajiri (Fedha). Huenda zipo sababu nyingi, lakini mimi nataka nikuonyeshe sababu tatu za kibibilia.
Sababu ya kwanza , kulinda mawazo na mikakati ya Mungu kwa watu wake.
 Yeremia 29:11. Mhubiri 7:12 “Kwa maana hekima ni ulinzi kama vile fedha ilivyo ulinzi na ubora wa maarifa ni ya kwamba hekima humhifadhi yeye aliyo nayo” Mithali 18:11 “ Mali ya mtu tajiri ni mji wake wa nguvu; Ni kama ukuta mrefu katika mawazo yake .
Kwenye kitabu cha Yeremia 29:11 Mungu anasema nayajua mawazo ninayowawazia, si mawazo mabaya, ni mawazo ya amani ………..Sasa ukiunganisha mawazo ya mhubiri 7:12 na mithali 18:11 utupata sentensi hii. Mungu anapokupa utajiri (fedha), anakutajirisha ili kulinda mawazo (mipango) na mikakati ya Mungu ambayo anakupa kabla ya kukupa hizo pesa kwa watu wake. Fedha yoyote ambayo Mungu anaileta mikononi kwako kumbe ina makusudi, mipango ya Mungu ndani yake.
Mungu anayo mipango na njia za kuwafanikisha watu wake kiuchumi, kimwili, kibiashara, kimaisha  n.k. sasa hii mipango inalindwa na nguvu ya fedha. Maana kama watu wake watakuwa masikini basi mipango aliyo nayo juu ya kanisa, familia, nchi n.k. basi si tu haitatekelezeka vizuri bali pia itanunuliwa na shetani kwa fedha yake. Hii ina maana Mungu anataka tuwe na nguvu ya kimaamuzi na ya utawala kwa yale anayotuagiza Mungu kwa sababu kwa fedha.
Sababu ya pili , Ili kuliimarisha agano lake.
kumbukumbu 8:18 Bali utamkumbuka Bwana, Mungu wako maana ndiye akupaye nguvu za kupata utajiri, ili ALIFANYE imara agano lake alilowapa baba zako, kama hivi leo.
Hapa tunaona wazi kabisa kwamba Mungu anasema ninakupa huo utajiri ili kulifanya agano lake kuwa Imara. Je agano hili ni lipi? Yeremia 31:31 inasema “Angalia, siku zinakuja, asema BWANA, nitakapofanya agano jipya na nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda, …. Nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaindika; nami nitakuwa Mungu kwao, nao watakuwa watu wangu.
Agano ambalo Mungu anataka uimarishe kwa fedha anayokupa ni la yeye kukaa na watu wake. Maana yake tumia fedha anayokupa kujenga na kuimarisha uhusiano mzuri kati ya Yesu na watu wake.Uhusiano wa Yesu kama mwokozi, Rafiki, mpanyaji, Bwana n.k kwa watu wake maana yake ni hii, tumia fedha kufanya jambo lolote maadamu una hakika litapelekea uhusiano wa mtu (watu) na Yesu kuimarika na jina la Yesu kutukuzwa. Na kwa sababu hiyo utukufu wa mwisho wa nyumba hii/agano hili utakuwa ni mkuu kuliko ule wa kwanza, Hagai 2:8
Sababu ya tatu, ili tukopeshe na sio kukopa .
Kumbukumbu la Torati 28:12 inasema Atakufunulia Bwana hazina yake nzuri … Nawe utakopesha mataifa mengi, wala hutakopa wewe .Sikiliza tumeshaona katika mithali 18:11 kwamba mali ya mtu tajiri ni mji wake wenye nguvu… kwa lugha nyepesi maana yake fedha ya mtu tajiri ni nguvu ya huyo mtu kwenye mji aliopo/ au ambao yupo. Kwa kuwa akopaye ni mtumwa wake akopeshaye, hivyo utakapokopesha maana yeke utakuwa na nguvu juu ya maamuzi na hisia za huyo au hao watu uliowakopesha.
kama tukibakia kukopa tutakuwa watumwa na kwa sababu hiyo ndiyo maana Mungu anatupa utajiri kwa mtu mmoja, familia, kanisa, nchi n.k
Naamini sehemu ya kwanza ya somo hili litakusaidia katika matumizi ya utajiri ambao Bwana Mungu amekupa.
Ubarikiwe

KWA NAMNA GANI MTU ANAWEZA KUMZIMISHA ROHO MTAKATIFU?


Roho Mtakatifuni Mungu, mwenye nguvu zote, maarifa yote, anayepatikana kila mahali. Yeye pia anayo nafsi na kwa hiari yake ameamua kuishi ndani ya mwili wa mwanadamu kwa kuzingatia mgawanyo wa majukumu waliyokubaliana yaani nafsi ya    Mungu Baba, Mungu Mwana(Yesu) na Mungu Roho Mtakatifu. Kazi/lengo kubwa la ujio wake ni kuwa Msaidizi wa mwanadamu kwenye ulimwengu huu wa mwili, ili kumsaidia kuishi katika mapenzi ya Mungu.
Mungu hana namna ya  kutawala kwenye ulimwengu wa kimwili bila kuwa na mwili wa damu na nyama, kwa kuwa yeye ni Roho (Yohana 4:24). Hivyo hana budi kuingia kwenye mwili wa mtu na kufanya makao yake hapo, ili kutawala na kumuongoza mwanadamu katika mapenzi yake (Yohana14:18, 23, 1Wakorinto 3:16-17, 6:19). Kwa sababu hii ni muhimu sana kwetu kutunza mahusiano yetu na Roho Mtakatifu ili tusimzimishe katika maisha yetu.
Paulo akizungumza na ndugu wa Thesalonike alisema ‘Msimzimishe Roho’ (1Wthesalonike 5:19). Paulo alitoa maonyo haya kwa kuwa alijua, Kumzimisha Roho Mtakatifu, kuna athari mbaya sana kwenye maisha ya mwamini katika kulitumikia kusudi la Mungu na hata maisha yake ya kawaida hapa duniani. Swali la msingi ni, kwa namna gani mtu anaweza kumzimisha Roho Mtakatifu? Ukisoma tafsiri za kiingereza, Biblia ya toleo la GNB katika mstari huu inasema Do not restrain the Holy Spirit’ na toleo la KJV linasema ‘Quench not the Spirit’ (1Th 5:19).
Tafsiri hizi mbili zinapanua zaidi tafsiri ya kumzimisha Roho, katika dhana mbili zifuatazo; moja kumzimisha Roho ina maana ya kumzuia Roho Mtakatifu asitawale na kuongoza maisha yako kwa kukataa msaada wake maishani mwako. Pili, kumzimisha Roho Mtakatifu ina maana ya kuishi katika mazingira ambayo yanamfanya Roho Mtakatifu ashindwe kukusaidia.
Mazingira ambayo Roho Mtakatifu anaweza kuzimishwa;
  • Kutokumpa nafasi akusaidie
Kwa mujibu wa Matahayo 14:16, Roho Mtakatifu ameletwa kwetu kama Msaidizi. Kwa tafsiri, Msaidizi ni yule atoaye msaada pale anapohitajika na kupewa nafasi ya kufanya hivyo. Vivyo hivyo na Roho Mtakatifu kama hujampa nafasi ya kukusaidia (ingawa yupo ndani yako), hawezi kufanya hivyo na kwa hiyo taratibu utakuwa unamfungia/unamzuia kukusaidia maishani mwako.
  • Kukosa upendo
Ukisoma kitabu cha 1Wakorinto sura ya 13 na 14, utagundua kwamba suala la upendo limepewa msisitizo wa kipekee kwa mtu ambaye anataka kuona utendaji wa kazi wa Roho Mtakatifu kwenye maisha yake na kwa ajili ya wengine pia. Upendo kwa mtu aliyejazwa Roho Mtakatifu ni moja ya vigezo muhimu sana kwa Roho Mtakatifu kusema/kujifunua na kufanya kazi ndani yako. Hivyo kukosa upendo ni dalili ya kumzimisha Roho Mtakatifu ndani yako. Ndiyo maana Paulo anasema hata kama angekuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, pia kuwa na imani timilifu kiasi cha kuhamisha milima, kama hana upendo si kitu yeye, naam ni bure tena ni ubatili (1Wakorinto 13:1-3).
  • Kuongozwa au kuenenda kwa mwili
Paulo aliwaambia hivi wandugu wa Galatia ‘Basi nasema, Enendeni kwa kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili’ (Wagalatia 5:16). Maneno haya alikuwa akiwaambia watu waliokoka na si wasiomjua Mungu. Kanisa la Galatia lilikuwa limeacha kuenenda kwa Roho likaanza kuenenda kwa mwili. Paulo akajua jambo hili litamzimisha Roho wa Bwana ndani yao, na kwa sababu hii hawataweza kuishi maisha ya ushindi hapa duniani na kisha kuurithi uzima wa milele, ndipo akawaonya akisema enendeni kwa Roho ili msizitimize tama za mwili.
  • Kutokutii maelekezo yake
Roho Mtakatifu kuitwa Msaidizi haina maana tunapaswa kumpamngia cha kufanya. Yeye ndiye mwenye kutuongoza katika njia itupasayo kuiendea (Zaburi 32:8). Kinachotakiwa ni mtu kuwa mtiifu kwa yale ambayo Roho Mtakatifu anakuagiza. Kukosa utiifu mara kwa mara kila anapokusemesha/kukuagiza ni kumjengea mazingira ya kutoendelea kusema na wewe na hivyo kuondoka kwako na kutafuta mtu mwingine amtumie kwa kusudi lake. 
  • Kukosa ufahamu wa utendaji wake
Mara nyingi watu wamemzimisha Roho kwa kutokujua utendaji wake ulivyo. Kuna nyakati Roho Mtakatifu anaweza akaleta msukumo ndani ya mtu wa kumtaka aombe, atulie kusoma neno n.k. Lakini kwa kutokujua namna anavyosema, wengi hujikuta badala ya kutulia na kufanya kile alichopaswa kufanya, wao hufanya mambo mengine.
Pia kuna nyakati katika ibada (sifa, maombi nk), Roho Mtakatifu anaweza akashuka juu ya mtu au watu na akataka kusema jambo, lakini viongozi wa makanisa au vikundi husika wakawazuia hao watu. Kufanya hivyo bila uongozi wa Mungu ni kumzimisha Roho. Mandiko yako wazi kabisa kwamba hatupaswi kutweza unabii (1 Wathesalonike 5:20) na wala hatupaswi kuzuia watu kunena kwa lugha (1Wakorinto 14:39). Zaidi tumeagizwa kujaribu mambo yote, na tulishike lililo jema (1 Wathesalonike 4:21).
Je tutajaribuje mambo yote ikiwa tunawazuia watu Kunena na pia tunatweza unabii? Hofu yangu ni kwamba kwa kuzuia watu kunena na pia kutweza unabii tunaweza tukajikuta tunamzimisha Roho Mtakatifu na kukataa uongozi wake kwenye maisha yetu. Ni vema tukakumbuka kile ambacho Paulo aliwaambia Wakorinto juu ya mambo haya kwamba ‘mambo yote yatendeke kwa uzuri na kwa utaratibu’ (1 Wakorinto 14:40). Naam na hili lina maana ni vema kwanza ujue utendaji wa Roho Mtakatifu ukoje, ili kuepuka kumzimisha kwa kutokujua utendaji wake.
Pengine yapo mazingira mengine ambayo mtu anaweza akajikuta anamzimisha Roho Mtakatifu. Kumbuka jambo hili kwamba kumzimisha Roho Mtakatifu ni kumzuia asikusaidie, jambo ambalo tafsiri yake ni kukataa uongozi wake kwenye maisha yako. Biblia inasema katika Warumi 8:9 ‘Lakini ikiwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu, ninyi hamwufuati mwili; bali mwaifuata roho. Lakini mtu awaye yote asipokuwa na Roho wa Kristo huyo si wake’. Usifanye mchezo na Roho Mungu hakikisha unatunza sana mahusiano mazuri kati yako na yeye kwa kutokumzimisha.
Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo iwe nawe

NAMNA YA KUMTUMIA ROHO MTAKATIFU KAMA MSAIDIZI KUPITIA KAZI ZAKE

Yohana 14:16-18 … Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni, wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu”.
Katika somo hili nataka kuandika juu ya kazi za Roho Mtakatifu na kukuonyesha namna unavyoweza kumtumia Roho Mtakataifu kama Msaidizi kupitia kazi zake. Labda niseme kwa lugha hii, kama unataka kuona msaada wa Roho Mtakatifu kwenye maisha yako, ni lazima kwanza uzijue kazi zake, maana kazi zake ndizo zinazotuonyuesha maeneo ya msaada wake, kazi zake ndizo zinazofafanua kwa namna gani Roho Mtakatifu ni Msaidizi.
Roho Mtakatifu ni nani?
Roho Mtakatifu ni Mungu, mwenye nguvu zote, maarifa yote, anayepatikana kila mahali. Yeye anayo nafsi na ameamua kuishi ndani ya mwili wa mwanadamu. Kusudi kubwa la ujio wake ni kuwa Msaidizi wa mwanadamu kwenye ulimwengu huu wa mwili, ili kumsaidia kuishi katika mapenzi ya Mungu.
Roho Mtakatifu amemamua kuishi ndani ya mwili wa mtu kwa sababu, Mungu hana namna ya  kutawala kwenye ulimwengu wa kimwili bila kuwa na mwili wa damu na nyama, kwa kuwa yeye ni Roho (Yohana 4:24). Hivyo hana budi kuingia kwenye mwili wa mtu na kufanya makao yake hapo, ili kutawala na kumuongoza mwanadamu katika mapenzi yake. (Yohana 14:23, Yohana 14:18, Ufunuo 3:20, 1Wakorinto 3:16-17, 6:19).
Kinachotusaidia kujua kwamba Roho Mtakatifu ana nafsi, ni tabia zake, maana kwenye kila nafsi kuna hisia, nia, kumbukumbu, akili nk. Baadhi ya sifa na tabia za Roho Mtakatifu ni; anapatikana kila mahali (Omnipresence), Zaburi 139:7, ana maarifa/anajua yote (Omniscient, Intelligence), 1 Wakorinto 2:10-11, ni mwenye nguvu zote/wa umilele (Omnipotent), Mwanzo 1:2, ni Mtakatifu, Luka 11:13, ana hisia (Waefeso 4:30, Mwanzo 6:3) – Wala msimuhuzunishe Roho wa Mungu…, Roho yangu haitashindana na Mwanadamu milele, ana nia (will), 1Wakorinto 12:11 – Hutenda kazi kama apendavyo.
 Kazi za Roho Mtakatifu
  • Kufundisha, Mwalimu (Yohana 14:26) … Atawafundisha yote…
  • Kuongoza, Kiongozi (Warumi 8:14, Yohana 16:13) – Atawaongoza awatie kwenye kweli yote, wote wanaoongozwa na Roho hao ndio … Mfano (Matendo ya Mitume 13:4, Acts 8:29)
  • Ni mfunuaji wa mambo/mafumbo/siri za Mungu (1Wakorinto 2:10) – Lakini Mungu ametufunulia sisi kwa Roho. Maana Roho huchunguza yote. Usipoteze muda kumtaka Mungu akufunulie siri zake, wewe mwambi Roho Mtakatifu hiyo ndiyo kazi yake.
  • Muombezi (Warumi 8:26) – Roho hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa.
  • Mtoa/mpasha habari za mambo yajayo (Yohana 16:13f) – Na mambo yajayo atawapasha habari yake.
  • Ni msemaji wa mambo ya Mungu/Yesu (Yohana 15:26, 2 Petro 1:21) – Yeye atanishuhudia (he will speak about me), Wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu wakiongozwa na Roho Mtakatifu.
  • Ni mtetezi/msemaji wa mambo yetu (Marko 13:11) – Kwa maana si ninyi msemao, bali ni Roho Mtakatifu.
  • Ni mkumbushaji wa yale uliyojifunza au uliyoagizwa na Mungu (Yohana 14:26)… Atawakumbusha yote niliyowaambia.
  • Kutia/kuwapa nguvu watu wake nguvu/uwezo (Matendo1:8) – Lakini mtapokea nguvu akisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu…
  • Kuuhakikisha (convict, make aware, sadikisha) ulimwengu kwa habari ya dhambi, haki na hukumu (Yohana 16:8) e.g unajuaje kwamba kuna hukumu? Warumi 8:16
Naam kazi hizi za Roho Mtakatifu zinatufikisha mahali pa kujua kwamba jukumu lake kubwa ni kuwa Msaidizi wa mwanadamu. Kufanyika msaada wa mwanadamu katika mambo hayo hapo juu pale mwanadamu atakapohitaji msaada huo.  Hivyo ni jukumu lako kumpa nafasi kwa kuboresha mahusiano yako na yeye ili akusaidie. Hata hivyo Roho Mtakatifu kuitwa Msaidizi haina maana kwamba ndio umvunjie heshima, bali fahamu kwamba, Roho Mtakatifu ni Msaidizi kwa namna ambayo bila yeye mimi na wewe hatuwezi kutenda neno lolote.
Kazi hizi zinatupa kujua kwamba Roho Mtakatifu yupo tayari kutusaidia katika kila eneo la maisha yetu. Ni jukumu letu kumpa  nafasi hiyo na kutambua kwamba bila msaada wake sisi hatuwezi lolote. Watu wengi leo hawaoni msaada wa Mungu kwao kwa sababu ya kutokumpa Roho Mtakatifu nafasi ya kuwasaidia katika maisha yao na pia kwa kutokujua maeneo ya kumtumia Roho Mtakatifu kama Msaidizi.
Je, unahitaji msaada wa Roho Mtakatifu eneo gani la maisha yako?, ni ndoa, kazi, madeni, huduma, kanisa, utawala nk mpe nafasi akusaidie, akufundishe na kukuongoza katika kweli yote. Kumbuka yeye ni Mungu ambaye ni Mwalimu na Kiongozi pasina yeye mimi na wewe hatuwezi neno lolote. Unataka kumjua Mungu, kuwa na maombi yenye matokeo mazuri na kufanikiwa katika maisha yako kiroho na kimwili pia mwambie Roho Mtakatifu akusaidie.
Msaada wa Roho Mtakatifu hauna mipaka maadam unahitaji msaada katika yale ambayo ni mapenzi ya Mungu. Hivyo haijalishi unapita katika jambo gani mpe nafasi Roho Mtakatifu akusaidie. Na ili uweze kuthamini msaada wa Roho Mtakatifu jifunze siku zote kufikiri kwa dhana kwamba bila msaada wake wewe huwezi lolote, na kwa sababu hiyo utaona umuhimu wa yeye kukusaidia katika maisha yako.
Usisubiri mambo yako yaharibike au usiachague mambo unayofikiri magumu ndio umshirikishe akusaidie, yeye anataka kuwa Bwana wa maisha yako, akusaidie kwa kila kitu hata mambo madogo kabisa kwenye maisha yako. Kina-muumiza Mungu kuona watoto wake chini ya jua wanahangaika katika maisha yao, wakati yeye amemleta Roho Mtakatifu ili awasaidie katika maisha hayo. Tumia vizuri fursa ya Roho Mtakatifu sasa maadam anapatikana, kuna wakati hatapatikana.
 Neema ya Kristo iwe nawe

Monday, October 8, 2012

KWA NINI UNATAKIWA KULITAFAKARI NENO LA MUNGU USIKU NA MCHANA?

                                                                        Na
                                                Mt. Meshack  Ezekia  Kitova
Yoshua 1:8 “kitabu hiki cha Torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo……..)
Hapa tunaona jinsi Mungu alivyomtisitiza Joshua kwa habari ya kulitafakari neno la Mungu usiku na mchana .
Lengo la waraka huu mfupi kwako mpendwa msomaji ni kukueleza sababu za msingi kwa nini ni lazima na sio ombi kwamba usome na kulitafakari Neno la Mungu usiku na mchana.Kabla sijakueleza sababu nikupe tafasiri ya Neno la Mungu kwa ufupi, neno la Mungu ni jumla ya mawazo ya Mungu juu ya mwanadamu.
Ndani ya Neno kuna maamuzi (hukumu), sheria, maagizo na njia za Mungu za kumtoa mwanadamu katika shida aliyonayo, kumfanikisha katika mambo yote na kumsaidia, kuishi kwa kulishika shauri (kusudi) la Bwana.
Sababu hizo ni ;
(a) uweze kuelewa nini mawazo ya Mungu juu yako .
Katika kitabu cha Yeremia 29:11 Mungu anasema nayajua mawazo ninayokuwazi si mawazo mabaya ………, sasa ili uweze kuelewa Mungu anakuwazia nini ni lazima usome kwa kulitafakari neno lake ili upate anachokueleza kuhusu maisha yako, huduma, kazi, biashara nk.
(b) upate kuifanikisha njia yako.
Yoshua 1:8b. Mungu anasema nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea ………….( Zaburi 32:8), kumbuka kila mmoja ana njia yake ya kupita ili kilitumikia shauri la Bwana. Sasa ili uweze kufanikiwa katika njia yako ni lazima usome na kulitafakari Neno la Mungu maana ni taa ya miguu yako. Zaburi 119:105.
(c) usimtende Mungu dhambi .
Zaburi 119:11. mwimbaji wa zaburi anasema, moyoni mwangu nimeliweka neno lako ili nisikutende dhambi. Neno linawekwa moyoni kwa kulitafakari. Kadri unavyolitafakari kimapana ndivyo linavyokusaidia na kukulinda na dhambi. Litakuonyesha hila na mitego ya dhambi ya shetani, na litakupa ushindi kwa kila ushawishi wa adui.
(d)Ili uongezeke kiimani.
 warumi 10:17. Ikiwa chanzo cha Imani ni kusikia, na kusikia huja kwa neno la kristo, maana yake kadri unavyolisoma na kulitafakari Neno la kristo mara kwa mara, kisha ukajitamkia mwenyewe ili ulisikie hii ina maana lazima imani yako itaongezeka tu.
(e)Neno limebeba jibu la mahitaji yako.
 Zaburi 107:20. kwa kuwa ndani ya neno kuna mawazo na njia (mikakati) ya kukufanikisha kimaisha, hii ina maana, unapolitafakari licha ya kuelewa mipango ya Mungu juu yako, pia utaelewa na njia za Mungu za kukuondoa katika shida uliyo nayo kiroho, kimwili, kindoa , kibiashara nk.
(f)uweze kustawi sana .
Yoshua 1:8b, Biblia inapozungumzia kustawi ina maana ya kutawala na kumiliki vema, kimapana yale ambayo Mungu ameyaweka chini yako .Mtu ambaye ndani yake amejaa Neno la Mungu kwa wingi huyo ana uwezo mkubwa sana wa kutawala na kuongoza watu pia.
(g)Litakupa miaka mingi duniani . Mithali 3:1. Ukilitafakari Neno la Mungu katika maisha yako.Neno litakupa miaka mingi ya amani (mafanikio) hapa duniani na kila ulifanyalo litafanikiwa.
(h)uwafundishe wengine kumjua Mungu.
 kumbukumbu 6:1-10. Mungu anataka watu wamjue yeye, kwa hiyo pindi unapotafakari anajifunua kwako, akajifunua kwako anataka uwaambie na wengine jinsi alivyo na ukuu wake ili wasimsahau yeye
Naamini baada ya kuwa umejua umuhimu wa kusoma na kutafakari Neno la Mungu usiku na mchana, utaamua kuanza pia kulisoma na kulitafakari usiku na mchana.

KUSIFU NA KUABUDU

                                                      na
                                         Meshack  Ezekia Kitova

Pamoja na ukweli huu wa sifa na kuabudu kuwa sehemu ya maisha ya mtu ya kila siku, bado kuna nguvu za ajabu pale waamini wanapomwimbia Mungu sifa. Huduma ya kumwimbia Mungu nyimbo za sifa na kuabudu, ndiyo huduma pekee ambayo mwamini hutumia nguvu na bidii nyingi, kupitia nafsi zake tatu. Kwanza, kupitia uimbaji mwamini hutumia nguvu kumpazia Mungu sauti yake, pili, hutumia viungo vya mwili wake kama vile mikono, miguu katika kucheza mbele za Mungu wa utukufu. Hali kadhalika katika kumwimbia Mungu sifa na kumwabudu, mwamini hutumia pia ufahamu kujihudhurisha mbele za Mungu mwenye maarifa yote. Bidii hizi zinazohusisha nafsi zote za mwanadamu, ndizo hatimaye zinazomleta mwamini karibu zaidi na nguvu na uwepo wa Mungu.
Katika kumsifu na kumwabudu Mungu, kanisa la Maranatha Reconciliation linaelewa kuwa, Roho Mtakatifu aliyemwagwa bila kipimo wakati wa Pentekoste ya kwanza baada ya ufufuko wa Bwana ni Roho wa sifa. Kiu yake kila wakati ni kuwaongoza waamini kumtolea Mungu sadaka ya sifa; mahali popote wanapokuwa ikiwa ni nyumbani, njiani, makazini, vitandani, kwenye maombi, wakati wa ibada n.k. Hata hivyo, kutokana na ukosefu wa mafundisho ya kutosha waamini wengi wameridhika na sifa na kuabudu kunakofanyika katika mikusanyiko ya ibada peke yake. Wakati umefika kwa watoto wa Mungu kuondoa vifusi vilivyoiangukia huduma hii na kuifanya ipoteze maana yake ya awali. Vifusi hivi vikishaondoka, kila mwamini katika nyumba ya Mungu atatambua kuwa, kusifu na kuabudu ni maisha na sio kuimba peke yake.
Hali kadhalika vifusi hivi vikishaondoka, waamini watatambua pia uhusiano uliopo kati ya kusifu na kumtolea Mungu shukrani. Ukiangalia mashairi ya mfalme Daudi, utagundua kuwa, nyingi ya Zaburi zake zinaongelea umuhimu wa kumtolea Mungu dhabihu za shukrani. Kwa mfano, tunapoangalia zaburi ya 116, tunakutana na shairi lifuatalo, "Nitakutolea dhabihu ya kushukuru; Na kulitangaza jina la BWANA." Zab 116:17. Katika kumsogelea Mungu ni sharti dhabihu hii ya shukrani itangulie kabla ya ile ya sifa na kuabudu. Ni katika hali ya kumtolea Mungu dhabihu ya shukrani ndipo Roho wa Mungu anapozimiliki nafsi tatu za mwamini na kumwongoza kumwadhimisha Bwana kwa bubujiko la ajabu, huku akitokwa na machozi ya furaha. Kutokana na uhusiano uliopo kati ya sifa, kuabudu na shukrani, ni sahihi kusema kuwa, ibada ya kweli ni lazima iwe na mambo makubwa matatu, KUABUDU, KUSIFU na KUSHUKURU.
Kwa maneno haya machache, tunayo imani kwa Mungu kuwa ataleta uamsho wa sifa na kuabudu kwa kweli katika kanisa lake hapa Tanzania. Wakati huu ambao uovu unaonekana kuimeza dunia, huduma hii ya kusifu na kuabudu kwa kweli, inahitajika sana katika kanisa. Huduma hii ndiyo itakayoweza kuziangusha ngome hizi za uovu. Ngome hizi zikishaanguka, ukuaji wa kanisa kitabia, kiidadi na kijiografia nao utashika kasi tofauti na ilivyo sasa. Mungu akubariki na akupe kiu na bidii ya kufanya huduma ya kusifu na kuabudu kuwa sehemu ya maisha yako ya kila siku. KILA MWENYE PUMZI NA AMSIFU BWANA, HALELUYA!

Kusifu na Kuabudu

Bwana asifiwe, mpendwa katika Bwana!
Napenda kukupa mambo machache kuhusu Kusifu na Kuabudu, ingawa nitalenga zaidi Kuabudu. Sababu inayonifanya niseme zaidi kuhusu Kuabudu ni kwa sababu kusifu na kuabudu ni safari inayoanza kutokea nje kwenda ndani. Kwa sababu hiyo kujua Kusifu bila kujua kuabudu ni sawa na kusafiri bila kufika mwisho wa safari.
Nitaanza kwa kuweka andiko. Ninaomba, ukiweza, usisome ujumbe huu kwa haraka bali soma kwa makini huku ukitafuta Mungu akufunulie zaidi. Andiko hili ni Mathayo 6:9 lisemalo, “Basi ninyi salini hivi, Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, Ufalme wako uje” Katika Luka 11 tunapata maneno kama haya ila kwenye mstari wa kwanza inasema kuwa Yesu alikuwa mahali akiomba na baada ya kumaliza mwanafunzi wake mmoja akamwambia, ‘Bwana tufundishe sisi kusali’. Inaonyesha wazi wanafunzi wake walivutiwa na sala za Bwana Yesu. Hapo ndipo Yesu anaanza kuwafundisha.
Watumishi wengi mbali mbali husema jambo ambalo nakubaliana nalo, kuwa huu alioonyesha Yesu ni muundo tu wa maombi au Kusali. Ombi au sala hii ni fupi sana kuwa tu ndiyo Yesu aliyofanya kwenye kufunga siku arobaini au kwenye masaa mengi ambayo Yesu aliomba mara kwa mara, asubuhi pia usiku.  Katika muundo huu wa sala sitaweza kuchukua vipengere vingi ila kimoja kinachohusu sana somo hili.
Yesu alionyesha sala au maombi yanatakiwa yaanze na kulitukuza Jina la Mungu. Kuingia uweponi mwa Bwana kunatakia kuanze kwa kusifu na kuabudu Mungu kisha mambo mengine yanayohusu maombi au sala yaendelee. Mwamini hawezi kuwa mwombaji au muombezi mzuri kama si mwepesi katika sifa na ibada. Tukikosa uangalifu katika hili ni rahisi tukaingia tu kuomba sana ikafika tukawa kama omba omba katika uwepo wa Mungu. Kuwa kila tunapomwendea Mungu tunaomba tu mahitaji yetu. Maombi na maombezi ni ya muhimu ila bila ya roho ya kusifu na kuabudu, maombi yetu yanaweza yajibiwe bila kumjua huyo Mungu anayeyajibu. Nasema hivi kwa sababu kujibiwa maombi na kumjua Mungu ni vitu viwili tofauti.
Watu kumi waliokuwa na ukoma walimlilia Yesu katika kitabu cha Luka 17:13, wakisema Ee Yesu, Bwana mkubwa, uturehemu”. Hilo lilikuwa ombi lao. Yesu akawaagiza waende kwa makuhani wakajionyeshe huko. Walipokuwa wakielekea huko, wakatakasika, wakapona ukoma uliokuwepo mwilini mwao. Kati yao ni mmoja tu ndiye aliyerudi kuonana na Yesu ili kumjua kibinafsi. Wale tisa walipata jibu la ombi lao bila kumjua mjibu maombi. Sitatenda haki hapa kama sitasisitiza hili kuwa kuna waombaji/waombeaji na wafanya sala wengi ambao kwa kukosa uelewa huu au kukosa kuzingatia jambo hili wameona miujiza mingi na majibu mengi ya maombi bila kumjua Mungu na njia zake. Siri za Mungu hufichuliwa sirini mwa Mungu. Ila majibu tu ya maombi, hata kwa kufunguliwa madirisha ya mbinguni, Mungu anaweza tu kuyashusha. Zaburi 91:1 inasema , “Aketiye mahali pa sirini pake aliye juu atakaa katika uvuli wake Mwenyezi”. Baada ya hilo kutimia, mistari inayofuata inaeleza kuhusu faida zake.
Nitakupa mifano michache kutoka kwenye maandiko ambayo watu waliomba na kupata jibu lakini bado Mungu hakuwa na ukaribu wa kujulikana. Kutoka 3:7, “Bwana akasema, hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko  Misri, nami nimesikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao…..”. Wana wa Israel walimuomba Mungu na akawasikia na kuwaonyesha matendo yake makuu na kuwatoa Misri. La ajabu ni kuwamba miujiza hiyo yote haikuwafanya wamjue Mungu. Waliendelea na uasi mpaka wakafa wote waliotoka Misri wakabakia Musa, Joshua na Caleb ambao ukiwatazama kwa makini utaona wao walimjua Mungu.
Luka 18 inaonyesha mama mmoja ambaye alimwendea kadhi dhalimu katika fumbo ambalo linamaanisha {katika mstari wa kwanza} kuwa watu wanapaswa Kuomba pasipo kukoma. Lakini kuna jambo la ajabu sana katika mstari ule wa saba (7) na nane(8): “Na Mungu je! Hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni mvumilivu kwao? Nawaambia atawapatia haki upesi; Walakini atakapokuja Mwana wa Adamu, je! Ataiona Imani duniani?
Nitaomba niishie hapo ili nirudi kwenye Kusifu na Kuabudu. Mungu akupe ufunuo hapo!
Kusifu ni kusema/kuongea au kutangaza sifa za mtu au kitu. Kumsifu Mungu ni kusema, kuongea au kutangaza matendo yake makuu.
Kuabudu ni kuwasiliana na Mungu kwa jinsi ya Yeye ni nani. Ni mawasiliano ya ana kwa ana, kati ya mtu binafsi na Mungu.
Katika kusifu siyo lazima mtu awe anawasiliana na Mungu. Hata kwa kuongea na mtu mwingine,  mtu anaweza akamsifu Mungu. Hata watu wasiomjua Mungu utawasikia mara kwa mara wakimsifu Mungu, kwa kusema ni mkuu kwa kuleta mvua na kadhalika. Lakini kuabudu inahusu mtu binafsi na uso wa Mungu. Kusifu hata kutoka mbali inawezekana, lakini kuabudu ni jambo la ana kwa ana.
Hebu tazama ibada tunazokuwa nazo  kwenye makanisa au mahali pa ibada. Wakati wa Sifa wahusika huwa wengi sana, na hata wasiomjua Mungu hujumuika. Lakini jambo la kusikitisha ni kwamba watu wanapotakiwa Kuabudu, kuingia patakatifu pa patakatifu, wengi hushindwa kuingia kabisa na hata hutamani kipindi hicho kiishe ili watu wafanye jambo jingine. Laiti vipindi hivi vya kuabudu vingekuwa virefu zaidi!
Mambo yote hapa duniani yatakoma: Kuomba, Maombezi, Kuponya wagonjwa, Kuhubiri, Kukemea pepo na kadhalika. Katika mambo ambayo yatadumu milele, mojawapo ni Kumsifu na Kumuabudu Mungu. Kwa nini basi kusifu na kuabudu kuchukuwe muda mfupi zaidi kuliko haya mengine katika ibada zetu?
Viongozi wa Kusifu na Kuabudu.
Ili usichoke acha nije kwenye wapendwa wanaohusika kuongoza vipindi hivi vya kusifu na kuabudu, baadaye nitarudi kumalizia.
1Mambo ya Nyakati 25:1, “Tena Daudi na maakida wa Jeshi wakatenga kwa utumishi baadhi ya wana wa Asafu, na wana Hemani na wa Yeduthuni, watakaotabiri kwa vinubi na vinanda na matoazi…..” Mstari wa 6, “Hao wote waliamriwa na baba yao, waimbe nyumbani mwa Bwana, wakiwa na matoazi, vinanda na vinubi kwa utumishi wa nyumbani mwa Mungu; Asafu, Yeduthuni na Hemani wakiwa wanaamriwa na mfalme”. Sifa na kuabudu wakati wa Daudi, mmoja wa watu waliojua siri ya ibada katika historia, halikuwa jambo la mzaha. Hapo juu tunaona jeshi lilihusika pamoja na mfalme kutenga wahudumu wa kuongoza sifa na kuabudu nyumbani mwa Bwana.
Ili Sifa na Ibada irudi vyema Kanisani au katika kanisa lolote, ni lazima kufanyike mambo  yafuatayo:
1.Wadau kanisani wahusike wote. Hapo juu tumeona serikali iliingilia kati kurudisha sifa na ibada nyumbani mwa Mungu. Lazima watumishi watafute uelewa wa Huduma hii na kuwekeza na kutafuta muda wa kutosha kuwafundisha na kuwafanyia semina viongozi wao wa Sifa na Ibada. Mahali kwingi waimbaji wa sifa wameachwa tu bila kupewa malezi ya kutosha. Wanatakiwa watafutiwe wataalamu wa kiroho na wa muziki, ili wapate uelewa mkubwa zaidi.
2.Viongozi wa Sifa na Ibada wajuwe kuwa kusifu na kuabudu si muziki na muziki sio kusifu na kuabudu. Wadau wengi wa kusifu na kuabudu wanafanya kosa hili na hivyo kukosea. Kusifu na kuabudu ni kitu kinachotakiwa kufanyika maishani mwetu kila mara, kuwe ama kusiwe na muziki! Viongozi wengi wa kusifu na kuabudu huwa wanaanza kuabudu wakija tu kanisani, wanapokuja kwenye mazoezi au wanapoanza kuongoza kipindi. Kiongozi wa kusifu na kuabudu anatakiwa ajae sifa na ibada katika maisha yake. Akisimama mbele ya watu aendeleze jambo ambalo analifanya mara kwa mara kwa mara katika maisha yake ya binafsi.
3.Kiongozi wa Sifa na Ibada ajue aina ya nyimbo zake. Mwimbaji wa nyimbo za kawaida kama za maadili na mwimbaji wa Sifa na Ibada wako tofauti. Kiongozi wa Kusifu na Kuabudu anatakiwa ajifunze kuimba nyimbo za Sifa na Kuabudu. Kuimba, kwa mfano, wimbo wa Daudi na Goliati kwa juma zima haitasaidia sana anapofikia wakati wa kuifanya huduma yake. Anatakiwa ajifunze na aweke nyimbo za Sifa na Ibada moyoni mwake.
4.Viongozi wa Kusifu na Kuabudu wachukuwe Huduma yao kwa mzigo (seriously). Sioni kwa nini mchungaji afunge na aamke saa tisa alfajiri ili kujiandaa kwa ajili ya kufanya huduma ya jumapili halafu wanaaomtangulia madhabahuni waamke saa mbili asubuhi! Kwa kutokujua uzito wa huduma yao, huduma ya kuongoza Sifa na Ibada imedharauliwa na wengi wamejikuta wakianguka kirahisi kutoka kwenye Huduma hii.
5.Viongozi wa Kusifu na Kuabudu wajilinde na kiburi. Ni heshima kumtumikia Mungu katika huduma yoyote na hivyo hakuna sifa zaidi katika kuongoza kusifu na kuabudu! Siku moja kiongozi wangu katika Kusifu na Kuabudu anayeitwa Lindh alimpata mtu anayetaka kujiunga na kikundi cha Kusifu na Kuabudu, akamuuliza kwa nini alitaka kujiunga na sisi, yule mtu alijibu “Nilikuwa shemasi na sasa naona Mungu anataka kuniinua”. Yule ndugu hakuruhusiwa kuingia kwenye kikundi cha Kusifu na Kuabudu kwa sababu hakujua anachotakiwa kufanya.
Mpendwa siwezi kuyasema yote ila napenda kukupa tu muhtasari wangu.
Yohana 4:23, “Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu”.
Labda mtu anaweza kuuliza, je! Nitajuaje kuwa sasa nimeanza kuwa na roho ya Kusifu na Kuabudu? Mambo yafuatayo yanaweza kusaidia katika kujitambua:
-Kusali kwako kutajaa Kusifu na Kuabudu, sio tu ‘maombi’. Kama unaweza kuomba masaa kumi, angalia ni mangapi kati ya hayo unatumia kusifu, kutukuza, kuabudu na kuliadhimisha jina la Bwana.
-Unaimba nyimbo za aina gani? Asilimia kubwa ya watu hupenda kuimba nyimbo za kujielezea hisia zao. Hapa siko kumpokonya mtu soko katika uimbaji wake au kanda yake. Lakini ni vizuri ukajua kuwa nyimbo zako zinaleta kitu gani katika maisha yako. Nyimbo za maadili ni nzuri lakini ni vizuri sifa zikajaa kinywani mwako maana Mungu hukaa katika Sifa za watu wake. (Zaburi 34:1)
-Huwa unafanya nini kanisani watu wanaposifu na kuabudu? Kama kila kipindi cha Kusifu na Kuabudu kinamchosha na kumkera mtu, basi hajaumbiwa bado roho ya Sifa na Kuabudu. Akichukua hatua nzuri, hiki kitu kitaumbika moyoni mwake.
-Unathaminije uwepo wa Mungu? Mtu anayependa kuabudu uwepo wa Mungu huwa unatembea naye na akishaonja utamu huo, hujaa hofu ya Mungu na hivyo hujitunza ili asiupoteze. Sijasema nguvu na upako, ila uwepo wa Mungu. Daudi ambaye alikuwa anaabudu sana alilia na kusema, katika Zaburi 51:11, “Usinitenge na uso wako, wala Roho yako mtakatifu, usiniondolee”. Musa naye akasema, katika kutoka 33:15, “….. uso wako usipokwenda pamoja nami, usituchukue kutoka hapa”. Ni jambo la ajabu Musa kuliomba baada ya miujiza yote ambayo Mungu aliwaonyesha wana wa Israel, na yeye mwenyewe akiwemo. Lakini alitaka uwepo wa Mungu binafsi, siyo tu matendo. Kuna utamu wa ajabu katika uwepo wa Mungu.
Na mwisho kabisa mpendwa, kuwa mwanafunzi wa kitabu cha Zaburi, ambacho Mungu kwa hekima yake alikiweka katikati kabisa mwa Biblia. Kitabu cha Zaburi kina maneno mengi ambayo ni njia mojawapo ya kupata lugha ya kumwabudu Mungu.
Basi, Mungu akipenda tutakuwa pamoja tena. Ubarikiwe sana!

Sunday, October 7, 2012

KUSUDI LA MUNGU … SASA!


Nilikuwa nikitazama filamu kuhusu Albert Einstein. Ikianza kulikuwa na kifungu kilichosema kitu kama, “Kila wakati baada ya mda mrefu sana, mwanadamu huja na kuona ulimwengu kupitia macho tofauti na kubadilisha ulimwengu anamoishi.” Tunataka kuweka changamoto hiyo mbele yako. Kuwa aina ya mtu yule ambaye Anaona ulimwengu, sio kupitia kwa macho ya kawaida, bali kupitia macho ya Kiroho. Pata changa moto ya kuwa mmoja wa watu wale ambao Waebrania 11 inawazungumzia kuwahusu. Ona maono ya Mungu ya makao ya Mungu na roho na utukufu unaoongezeka daima. Ona picha katika macho ya akili yako, kama inavyosema kwamba waumini katika kitabu cha Waebrania 11 walivyo ona. Waliona Mji ambao Mjenzi na Mtengenazaji alikuwa Mungu, na kwa hivyo hawakurithika na kitu kingine chochote. Hawakuwa tayari kurudi mji wa zamani. Waliona Mpango wa Mbinguni kwa mbali, na hata kama hawangeweza kuishika na mikono yao, hata kama hawangeweza kuishi ndani ya Mji huo ambao Mungu aliwapangia, hawakuwa tayari kurudi nyuma. “Kwa hivyo, Mungu hakuona haya kuitwa Mungu wao na hao watu Wake.”
Chango moto hiyo moja iko mbele yako wewe na mimi. Angalia dunia unayoishi, ulimwengu unamoishi, na haswa “kanisa” ulilo ndani yake na utamani Nyumba ya Baba ikuchukue. Na tamaa Yake ikuchukue kwa njia ambayo utakuwa tayari kuhatarisha kila kitu katika maisha yako ndiposa uone hiyo ikikamilika katika mazingira yako. Unaweza kuhatarisha maisha yako. Unaweza kuhatarisha familia yako (Zaburi 69:8-9). Unaweza kuhatarisha kazi yako. Unaweza kuhatarisha kila kitu kwa ajili ya Mungu na madhumuni Yake. Hapo ndipo tunapotoka. Kuzungumza Kibiblia hiyo kwa kweli ndiyo aina ya pekee ya Ukristo uliopo. Hilo si fikra au wazo linalojulikana sana. lakini katika Warumi 4 inasema , “Wale waliyo na imani ya Ibrahimu ni wana wa Ibrahimu.”
Kwa hivyo, haijalishi hali yoyote ile au kanisa ulioko, na mahali unaweza kuwa ( nchi yoyote au makao ambayo unayo na uitayo nyumbani kwa sasa), unastahili kuwa mwangalifu sana ili usikubali chochote ambacho Mungu hakubali. Usikubali kwa ajili ya uvivu, kutokujua Neno la Mungu, au ukosefu wa maono au dhambi katika maisha yako ya kibinafsi ambayo imekuziba au kukujeruhi hadi unahisi hautoshi. Usiruhusu wengine ambao wametoshelezwa na Lao wakusaliti au kukukejeli ili uwe fugufugu.
Pengine umeuziwa ukweli kwamba wewe ni “walai” tu na hauna chochote cha kutoa. Pengine unadhania maoni yako hayana umuhimu kwa sababu kuna watu wengi huko nje wenye hekima na waliosoma… “Wewe unajua Ni nini?” Ninataka kukuhimiza kwamba haijalishi wewe ni nani, una kitu cha kutoa. Ikiwa kwa kweli umeitwa kwa jina la Bwana na umemwuliza achukue usukani wa maisha yako, una kitu cha kutoa. Ikiwa umemwuliza akuoshe dhambi zako, una kitu cha kutoa. Haja Yake ni kwamba kuanzia mdogo hadi mkubwa na kila mtu amjue Yeye, aishi katika baraza Lake na ashiriki na Yeye, na Utatu, kila siku.

Mara moja baada ya muda mrefu sana, mtu huja au watu huja ambao wako tayari kushuku ulimwengu wanamoishi na kufanya utofauti katika ulimwengu ulio karibu nao. Waebrania 11 inahusu hiyo. Hiyo ndiyo Mungu ameitia kila mmoja wetu awe ikiwa tuna ujasiri na tuko tayari na tunaushirika na kichwa. Tukikaa ndani Yake, kutakuwa na matunda ya kuonyeshana. Unaweza kuwa mtu ambaye analeta utofauti katika ulimwengu ulimokuwa.
Ninatumaini tumeweka wazi kuto kuelewa moja ambayo imengia katika jamii ya Wakristo. Hiyo ni kwamba kuwa Mkristo ndio mwisho wa hadithi. Na kisha “kuhudhuria kanisa unalolipendelea Jumapili” ni udumishaji hadi Yesu arudi tena na wewe uende kwa nyumba ya kifahari juu ya mlima. Ninataka kuliondoa wazo hilo kabisa kwa sababu hilo si wazo la Mungu. Mungu anaita wazo hilo dini la uongo na Laokia, ambalo linatatiza tumbo Lake.
“Kusudi la Mungu ni kwamba sasa, kupitia kanisa, hekima ya Mungu iliyo ya namna nyingi ijulishwe viongozi na wenye mamlaka katika ufalme wa mbinguni….” Waefeso 3:10
Hili ndilo kusudi la Mungu SASA HIVI. Mapenzi Yake ni kufanya hekima Yake iliyo ya namna nyingi ijulikane kupitia Kanisa. Sio kupitia watu ambao wameokoka, na wala sio kupitia jamii ya watu wasiyo weza kuzaa ambao wanasikiliza mahubiri siku maalum ya wiki wakiwa wamevaa suti na tai… lakini kupitia kitambaa cha maisha, kupitia jamii ya waumini ambao “wameunganishwa na kushonwa pamoja na kila kano ya kushikilia,” na watu ambao vipawa vyao vimeunganishwa sana, hao “wanashirikiana.” Kuunganishwa, kwa “moyo mmoja, akili moja, kukubaliana pamoja, na kusudi moja.” Pigania maono hayo kwa Matendo ya waumini kutochukua mali, kwa kuunganishwa pamoja—kwa “kujitolea kwa mafunzo ya mitume, kumega mkate, kushirikiana, maombi,” na “kila siku hadharani na kutoka nyumba hadi nyumba.” Fikiria Watu wa Mungu kama ushirika—uliounganishwa, ulio na kitambaa cha maisha cha pamoja ambacho milango ya kuzimu haiwezi kuishinda. Dini ambalo msingi wake ni “mahudhurio” ni sawa kwa Waindi na Waislaamu, lakini sio ile Yesu aliyonzisha na kupaka mafuta.
Kusudi Lake ni “sasa, kupitia Eklesia,” kupitia Ushirika ambao ni wa kweli na wala sio umati wa watu ambao wanahudhuria kitu, bali maisha ambayo yameunganishwa—“kuungamiana dhambi,” kubebeana mizigo” na “kupendana.” Hiyo ndio aina ya maisha ambayo wanadamu wanaweza kuona. Hayo ndiyo aina ya maisha ambayo Yesu alizungumzia kuhusu wakati aliposema “kwa upendo wetu sisi kwa sisi” kuwa “watu wote watajua” imetoka mbinguni (Yohana 13). Alisema kwamba hiyo inaweza “kuaibisha ufalme na mamlaka.” Kusudi la Mungu ni sasa “kupitia Kanisa” ili kuleta aibu hadharani kwa shetani na falme na mamlaka yote. Na kusudi Lake, kulingana na maandiko, ni “SASA” kupitia kanisa ili kuwafanya Adui wake wawe chini ya miguu yake—sio tu kuja Kwake kwa pili na Ufalme mkuu wa Milele, kazi ya Mungu iliyokamilika, bali SASA.
                   Na kwa hakika, hatuzungumzii juu ya jamii kamili. Hatuzungumzii kuhusu sera za jamii, wala sio jambo la baada ya milenia, sio masomo ya utawala. Sio kunyumbua misuli, bali kando na hayo… Tunazungumza kuhusu Watu wakionyesha Maisha ya pamoja kwa njia moja na vile Yesu alionyesha maisha Yake, kama Mfalme wa wafalme wote. Alizaliwa mtoto wa haramu horini, akipanda punda aliye azimwa, na hakuwa na mali yoyote Yake—hakuwa na nguvu, hakuwa na elimu, hakuwa na jukwaa la kisiasa, hakuwa na “urembo au ukuu ambao mtu yeyote angevutiwa.” Tunazungumzia kuhusu kuwa mpenda watu aliyetoka mashinani ambaye angeweza kuona mioyo ya watu na kuwaleta msalabani. Tunazungumza kuhusu kuonyesha watu kashfa ya kuwepo Kwake na maisha Yake, na kuwaita wawe wavuvi wa watu. Wawe sehemu ya Nyumba Yake, “makao” Yake. Wawe mawe yaliyohai. “Ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa.” Huo ndio moyo wa Mungu.

                    Pokea Yesu wa Nazareti, na Ufalme “usio wa ulimwengu huu”, sio kama mshinda Roma au nchi yoyote tunamoishi, au mfumo wa “kanisa.” Mpokee kama Mfalme Seremala aliyependa, na kusemehe, na kutoa maisha Yake…. na yule aliyekuwa tayari kupindua meza za hekalu na kutoa fimbo kama ingehitajika kwa upendo wa Baba Yake na kwa ajili ya Nyumba ya Baba Yake.
Yesu alikuwa tayari kushuku ulimwengu alimokuwa na kwa hivyo kuibadilisha, na ametuita tuwe watu wa aina hiyo. Hii si upitishaji wa habari. Huu ni mwito wa utakatifu na utakaso wa madhumuni ya Mungu, na mwito wa kuinua maono Yake katika mioyo yenu na katika maisha yenu. Piga magoti na uombe. Huu ni mwito, si wa kubadilisha ulimwengu unao onekana tu, bali pia kubadilisha ulimwengu usionekana. “Kusudi Lake ni sasa kupitia Kanisa ili hekima Yake ijulikane, hekima ya Mungu iliyo ya namna nyingi, kwa falme na utawala” na kwa watu wote….
Kwa hivyo, hebu kaa linalochoma lisafishe midomo na moyo wako, mwangalie Mungu, na umlilie “Niko hapa, nitume!”